Usaid yaahidi kuendelea kusaidia waandishi

 Na Seif Mangwangi ,Arusha

MAAFISA wakuu wa mfuko wa maendeleo wa Marekani (USAID) kupitia ubalozi wake hapa nchini, wametembelea ofisi ya  Chama Cha Waandishi wa habari Arusha na kuahidi kuendeleza mahusiano na Chama hicho.

Akizungumza katika kikao Cha pamoja na watendaji wa APC, Mkuu wa idara ya Maendeleo ya USAID anayeshughulikia kitengo Cha Haki za Binaadam, Demokrasia na Utawala Bora  Steve Andoseh amesema amefurahishwa na namna APC imeweza kutekeleza miradi mbalimbali chini ya ufadhili wa fedha za walipa kodi wa Marekani.

Amesema USAID imekuwa ikitoa kipaumbele kwenye miradi ya Demokrasia, Haki za Binaadam na Utawala Bora kwa kuwa  wanaamini mambo hayo yakiwekwa sawa wananchi watapata maendeleo kwa wakati.

Andoseh amesema amefurahishwa na uhusiano uliopo kati ya Jeshi la Polisi na waandishi wa habari kufuatia hatua ya APC kuendesha midahalo na Jeshi hilo kupitia mradi wa IMS unaoratibiwa na umoja wa klabu za waandishi wa habari Tanzania (UTPC).

Kwa upande wake Afisa Programu wa mfuko huo nchini, Adam Lingstone ameipongea APC kwa kusimamia vyema mradi wa DDA na kusababisha mabadiliko ya Sheria kandamizi za habari.

Amesema pia kupitia mradi huo waandishi wa habari wanaofanyakazi zao kupitia mtandaoni wameweza kupewa mafunzo mbalimbali ya kuwajengea uwezo wa umahiri katika uandishi wa habari.

Awali akiwasilisha Taarifa ya APC, Mratibu  wa APC ambaye pia ni Afisa Programu katika mradi wa DDA, Seif Mangwangi amesema mafanikio mengine ya mradi wa DDA ni kuwezesha kuanzishwa kwa taasisi ya kusimamia maslahi ya waandishi wa habari mtandaoni, (TOMA), ambayo inatarajiwa kuzinduliwa hivi karibuni.

Amesema kupitia mradi wa DDA, baadhi ya waandishi wa habari mtandaoni wameweza kutumia vizuri mafunzo waliokiwa wakipata na matokeo yake ni kupata tuzo za umahiri katika uandishi.

” Miongoni mwa waandishi waliojengewa uwezo na mradi wa DDA na kupata tuzo za uandishi Bora ni pamoja na Joseph Mwaisango, Bakari Chijuba, Mohamed Zengwa, George Binagi, hawa na wengine wengi wamekuwa tangu mwanzo wa mradi ambao wanatambulika kama alternative media,”amesema.

Mtendaji Mkuu wa taasisi ya Freedom House, Wakili Daniel Lema amesema, APC imekuwa mfano wa kuigwa kati ya taasisi za kihabari nchini kutokana na utekelezaji mzuri wa mradi wa DDA ambao unatarajiwa kumalizika Septemba mwaka huu 2023.

Hata hivyo amesema, taasisi yake itaendelea kuijengea uwezo APC katika nyanja mbalimbali ikiwemo utayarishaji wa mpango mkakati ambao utaelezea malengo ya Chama kwa kipindi flani.

” Nawapongeza sana APC kwa wasilisho zuri kuhusu utekelezaji wa miradi mbalimbali, Freedom House tunajivunia uwepo wenu na mmekuwa mfano wa kuigwa, pamoja na kwamba mradi wa DDA unafikia mwisho lakini tutaendelea kuwajengea uwezo kwenye maeneo mengi hasa ya uandishi wa mpango mkakati na usimamizi wa miradi,”Amesema Lema.

Kwa upande wake Makamu Mwenyekiti wa bodi ya Wakurugenzi ya APC, Mussa Juma amesema APC Iko kwenye hatua za mwisho za kukamilisha mpango mkakati lakini kabla ya kuufanya kuwa rasmi tutawasiliana na taasisi ya Freedom House kwaajili ya kuuweka sawa.

Amesema malengo ya APC ni kuwa na kituo  kikubwa cha redio na televisheni mtandaoni, ili kuwapatia ajira wanachama wa APC lakini pia kujipatia fedha za kuendesha ofisi.