Dc arusha awahakikishia maslahi wenyekiti katika zoezi la anwani za makazi

Mkuu wa Wilaya ya Arusha, Said Mtanda

 *Asisitiza uwajibikaji, kumaliza kazi kwa wakati 

*Atakaye hujumu zoezi kufikishwa maadili, kuchukuliwa hatua

Na Seif Mangwangi, Arusha

Watendaji wa kata, mitaa na wenyeviti wa mitaa mbalimbali ya jiji la Arusha wametakiwa kuongeza kasi ya uandikishaji wa anwani za makazi ili liweze kumalizika kwa muda uliopangwa.

Aidha watendaji ambao watabainika kuhujumu zoezi hilo Serikali imesema itawachukulia hatua kali za kinidhamu na kuwafanya mfano dhidi ya wengine watakaokuwa na nia hiyo ovu.

Akizungumza leo Februari 25 kwenye kikao kazi kilichoshirikisha wenyekiti wa mitaa, watendaji wa kata na mitaa pamoja na maafisa Tarafa Mkuu wa Wilaya ya Arusha Said Mtanda amesema zoezi linalofanyika ni la kitaifa na limepewa baraka zote na Rais Samia Suluhu Hassan hivyo kila mmoja anatakiwa kuliheshimu.

“Zoezi hili limetolewa muda maalum wa kulimaliza na sote tunajua tulishaelezana, nawaomba sana msije kulihujumu, nimesikia kuna baadhi ya wenyeviti wanazembea, nyie hata kama sio waajiriwa ila mimi nitapambana na yeyote atakayehujumu hili zoezi, mimi ni mjumbe wa kamati ya maadili ndani ya CCM na wewe kwa kuwa umechaguliwa kupitia CCM ukiharibu huko chini utaletwa kwangu na mimi nitakushughulikia,”Ameonya.

DC Mtanda amesema amewahakikisha viongozi hao kuwa watalipwa stahiki zao ili kuwapa motisha ya kazi na kumwagiza Mkurugenzi wa Jiji la Arusha Dkt John Pima kuharakisha malipo ya posho za viongozi hao.

Mkurugenzi wa Jiji la Arusha Dkt John Pima

Mkurugenzi wa Jiji la Arusha Dkt John Pima amesisitiza uadilifu katika zoezi hilo na kusema wenyeviti na watendaji hao ndio msingi mkubwa wa mafanikio ya zoezi hilo na kwamba endapo hawatatoa ushirikiano zoezi zima litashindikana.

Amewataka kuichukua kazi hiyo kwa uzito wa hali ya juu ili kuimaliza kwa haraka lakini pia kuipatia sifa Jiji la Arusha mbele ya Rais Samia Suluhu Hassan ambaye amesisitiza sana kukamilishwa kwa kazi hiyo kwa wakati lakini kwa ufanisi wa hali ya juu.

kwa upande wake mmoja wa waratibu wa zoezi hilo Jiji la Arusha, ambaye pia ni afisa  mipango miji,  Doroth Absalom  amesema pamoja na changamoto chache zilizojitokeza awali lakini zoezi hilo la uhakiki wa majina ya mitaa na barabara na uandishi wa namba  limeenda vizuri kwa awamu ya kwanza.

”  Zoezi limeenda vizuri sana na hivi sasa vijana wanakamilisha fomu walizozigawa na kuingiza kwenye mtandao takwimu hizo, nyumba zote tumeweka alama kwa chaki baadae tutarudi kuanza kuziandika sasa kwa wino,”amesema.

kwa upande wake Mwenyekiti wa Mtaa wa Sanawari kata ya Sekei Dominick Maji amesema zoezi katika mtaa wake limeenda vizuri licha ya changamoto chache zilizopo ikiwemo kuchelewa kujazwa kwa fomu.

“Mimi kwangu nimegawa fomu zaidi ya 300, makazi ya polisi ambayo yapi kwenye mtaa wangu wenyewe nimewapa fomu 180 pekee na hawa ndio ambao  wanaonikwamisha bado hawajajaza hizi fomu, ila najaribu kuongea na wakubwa zao watajaza tu, “anasema.

Wenyekiti wa mitaa,kata na watendaji wakisikiliza hotuba ya Mkuu wa Wilaya ya Arusha Said Mtanda (hayupo pichani), alipokuwa akiwasihi kumaliza kazi ya anwani za makazi kwa wakati

Rahabu Mwakatobe mwenyekiti wa mtaa wa National Housing  na chrisanta Mwinyimvua mwenyekiti wa mtaa wa TCA Ngarenaro, wanasema maagizo yaliyotolewa na Mkuu wa Wilaya wameyachukua na watatekeleza zoezi hilo kwa haraka.