Ukame waathiri uvuvi na na ufugaji:malema

 Na Doreen Aloyce, Dodoma

MKURUGENZI Msaidizi ,Uendeshaji mazao , pembejeo na Ushirika Wizara ya Kilimo na chakula, Beatus Malema amesema mabadiliko ya Tabia nchi ambayo yamesababisha hali ya ukame hapa nchini, imekuwa tishio kwa upande wa uvuvi na ufugaji.

Beatus ameyasema hayo leo jijini Dodoma kwenye ufunguzi wa warsha ya Kitaifa na mkutano Mkuu  wa kwanza wa wanachama wa Shirikisho la vyama vya wakulima wadogo Tanzania (SHIWAKUTA).

Amesema kuwa kuwepo wa mabadiliko hayo ya Tabia nchi yameleta madhara kwa wafugaji,wakulima na wavuvi ikiwemo kupungua kwa mvua,kunyesha pasipokuwa na mtiririko wa kawaida  hali inayopelekea wakulima kushindwa kupanda mazao yao kwa wakati.

Amesema kupitia hali hiyo serikali imekuwa ikiwasisitiza wakulima kukata  nyasi na kuzitunza wakati wa masika ili waweze kuzitumia vizuri wakati wa matokeo ya kiangazi hasa kulishia mifugo .

“Kumekuwepo na mabadiliko ya Tabia nchi ambayo yanapelekea kuathiri wakulima na wafugaji lakini tumekuwa tukiwashauri kupanda mazao yanayostahimili ukame,na yale yanayokomaa mapema hasa uwele,mtama,viazi vitamu kwa hapa Dodoma huku tukiwasihi kutunza vyanzo vya maji ’’amesema

Aidha  akizungumza ndani ya mkutano huo amewataka viongozi wa chama hicho kuendesha chama kwa maslahi ya wanachama na sio wao binafsi kwani mara nyingi amekuwa akipata malalamiko kuhusu vyama kuendeshwa bila kufuata kanuni na kukiuka matakwa  matokeo yake wanachama kuwakimbia .

Kwa upande wake Mratibu wa Mpito wa Chama hicho cha SHIWAKUTA ,Richard Masandika amesema chama hicho ni Taasisi mpya ikiwa na lengo la kuvileta pamoja vyama vya wakulima vya Tanzania vilivyosajiliwa kama jumuia za kijamii zikiwa zinafanya kazi za uzalishaji katika kilimo,ufugaji,na uvuvi .

Pia amesema wamejipanga kuwajengea uwezo wa uzalishaji wa masoko ,kutoa taarifa huru,zinazoaminika zenye msingi wa Ushahidi ,ushauru na uchechemuzi juu ya maslahi ya wazalishaji wadogo.

‘’SHIWAKUTA ilisajiliwa Rasmi mwezi juni mwaka 2021 ambapo makao makuu yapo Arusha lengo kuu likiwa ni kuwaleta pamoja wakulima wadogo ili kulinda maslahi yetu  na tuna mikakati mbalimbali ikiwemo kujenga uwezo wa shirikisho kutekeleza kazi na wajibu wake ,kujishughulisha na sera,sheria zinazohusiana na kilimo,ufugaji , uvuvi ,ardhi na maliasili kwa ajili ya hali endelevu za jamii’’amesema Masandika.

Nae  Mwenyekiti wa chama hicho,Marcelina Kibena ameiomba Serikali kuangalia namna ya kufanya kazi kwa ukaribu na wazalishaji wadogo vijijini kupitia vyama vyao .

‘’mifumo ya uzalishaji wa chakula nchini umehodhiwa na wazalishaji wadogo vijijini tunaomba serikali ifanye kazi na wazaliushaji wadogo  kwa ukaribu katika kuendeleza mfumo wa kilimo cha kiikolojia na itasaidia nchi yetu kupata suluhisho endelevu kukabiliana na mabadiliko ya tabia nchi na usalama wa chakula .