Maofisa watendaji wa kata arusha watakiwa kuandaa mpango wa maendeleo wa kata unaoendana na mahitaji ya wananchi

Maofisa Watendaji wa Kata, halmashauri ya Arusha wametakiwa kuandaa Mpango wa Maendeleo wa kata, unaotekelezeka na unaoendana na mahitaji ya wananchi ili kuweka malengo makakati ya utekelezaji wa mapngo huo, kwa maendeleo wananchi wa kata hizo.

Rai hiyo imetolewa na Mkurugenzi Mtendaji, halmashauri ya Arusha, Saad Mtambule, alipofanya ziara yake ya kwanza ya kikazi ya kutembelea Ofisi za kata za halmashauri hiyo, kujionea  utendaji kazi wa ofisi hizo, pamoja na uibuaji wa miradi ya maendeleo katika maeneo hayo.

Mkurugenzi huyo, amewataka Maofisa Watendaji zote za halmashauri hiyo, kuwa na Mpango wa Maendeleo kisekta, unaotokana na maoni na mapendekezo ya wananchi, ukijikita kwenye changamoto zinazoikabili jamii husika pamoja na mipango mkakati wa kuzitatua kwa kuzingati vipaumbele vya wananchi hao.

Aidha amefafanua kuwa, Mpango huo wa Maendeleo, utawezesha kuandaa bajeti ya mwaka kulingana na mahitaji ya jamii,hasa kwa kuzingatia vipaumbele vya wananchi wa maeneo hayo.

“Mpango wa Maendeleo wa Kata ndio Dira ya Maendeleo ya Kata, utakaowezesha Maofisa Watendaji wote, kupanga utekelezaji wa shughuli zote za maendeleo kwa mwaka na kufanya tathmini yakufahamu mwelekeo wa maendeleo walipotoka, walipo na malengo wanayotarajia kufikia kwa kuzingatia maendeleo ya kiuchumi na kijamii” amesisitiza Mkurugenzi huyo.

Ameendelea kufafanua kuwa Mpango huo wa Maendeleo, utawawezesha wananchi pia kufahamu vema dira ya maendeleo katika maeneo yao, na kujipanga namna ya kushiriki kutatua changamoto zinazowakabili kwa kuzingatia vipaumbele vyao na Taifa kwa ujumla.

Aidha amewataka Watendaji hao kukaa na Watendaji wa vijiji pamoja na  wataalam wote wa ngazi hizo, kuandaa Mpango huo wa Maendeleo kisekta, kwa kuzingatia mahitaji ya wananchi katika maeneo yao, sambamba na kupata maoni kupitia wajumbe wa serikali za vijiji na mikutano ya vijiji. 

Naye Kaimu Afisa Mipango, halmashauri ya Arusha, Albert Mahoo, Mpango wa Maendeleo ya kata unaanza kwa kukusanya mapendekezo ya mahitaji ya  wananchi kisekta kupitia mikutano ya vitongoji na vijiji, kisha kuandaa mpango huo kupitia ofisi za kata kwa kuzingatia mpango halisi wa bajeti na vipaumbele kisekta.

Ameongeza kuwa, Mpango huo wa maendeleo, utawawezesha Watendaji wa kata na vijiji kuandaa bajeti inayoendana na mahitaji ya jamii husika na kurahisisha ushiriki wa jamii katika utekelezaji wa shughuli za maendeleo katika maeneo yao, na kufungua njia kwa wadau wa maendeleo kushiriki utekelezaji wa miradi ya maendeleo katika maeneo husika.

Awali Mkurugenzi Mtendaji halmashauri ya Arusha, amefanya ziara ya kutembelea kata za Moivo, Oloirieni na Olturumet lengo likiwa kuhakikisha utendaji wa kazi kuanzia ngazi ya kata, uendane na Mipango wa maendeleo wa halmashauri na taifa.