Jamii imekumbushwa kumlinda mnyama kakakuona

Kakakuona, mnyama ambaye kwa mujibu wa utafiti uliofanywa na Shirika la Tanzania Research and Conservation Organizations (TRCO)anatajwa kuwa yupo hatarini kutoweka (Picha kwa hisani ya Mtandao)

Egidia Vedasto, APC Media,

Arusha.

Jamii imekumbushwa kumlinda mnyama Kakakuona hususani jamii zinazoishi maeneo yanayozunguka shoroba mbalimbali hapa nchini.

Akizungumza na baadhi ya wadau wa uhifadhi wa wanyamapori kutoka mkoa wa Manyara, Mratibu wa Mradi wa Kuhifadhi Kakakuona shoroba ya Kwakuchinja ambaye pia ni Meneja rasilimali watu na Utawala mmoja wa waanzilishi wa Shirika la  Tanzania Research and Conservation Organizations (TRCO) Elisante Kimambo, amesema kuna faida nyingi iwapo mnyama Kakakuona atatunzwa vizuri.

Mafunzo ya kukuza uelewa kuhusu biolojia, ikolojia na uhifadhi wa kakakuona kwa wakazi wa kijiji cha Kwemtindi.(Picha Kwa hisani ya TRCO)

Ameeleza kuwa, Kakakuona mmoja anakula wadudu kama siafu na mchwa wapatao milion 70 kwa mwaka ambapo kwa kufanya hivo inafanya wadudu wasiongezeke sana kupita kiasi na kuonda adha hiyo kwa binadamu na mali zao. 

Aidha ameeleza kuwa, Kakakuona ni mnyama adimu anayetakiwa kulindwa kwani zipo aina nane tu duaniani na Kwa nchi ya Tanzania zipo aina tatu ambazo ni Kakakuona mkubwa, kakakuona wa ardhini pamoja na Kakakuona mwenye tumbo jeupe.

Hatua hiyo inatokana na utafiti uliofanywa na Shirika hilo kwa kipindi cha mwaka 2022/2023 na kuja na matokeo yanayoonyesha mnyama huyo yupo hatarini kutoweka iwapo juhudi za haraka hazitachukuliwa.

Wadau wa uhifadhi wakifuatilia uwasilishaji wa utafiti juu ya kakakuona uliofanywa na Shirika la Tanzania Research and Conservation Organizations (TRCO)

“Nitoe angalizo kwa wananchi, ukimuona Kakakuona usimuue, mshike mkague kama ana jeraha au shida yoyote, toa taarifa haraka kwa mamlaka inayokuzunguka kwa maana ya mwenyekiti au mtendaji wa Kijiji au mtaa au kwa Afisa wanyamapori au daktari wa wanyamapori au mifugo aliye karibu”

“Wakati unasubiria huduma kutoka kwa mamlaka husika, hakikisha huyo Kakakuona hapati usumbufu wa makelele na kuguswaguswa na watu wengi”

“Ikiwa hana shida yoyote basi unaweza kumrudisha maeneo yenye majimaji na uhakika wa wadudu ili asitafute chakula chake kwa muda mrefu,  asifungiwe kwa muda usiozidi siku mbili kabla ya kurudi kwenye mazingira yake” amefafanua Kimambo.

Ameendelea kufafanua kwamba Kakakuona ni mnyama mpole hivyo hana madhara yoyote kwa jamii hivyo kuwasihi wananchi kutomdhuru pindi wanapomuona akiwa katika shughuli zake.

Amewataka wananchi kutomuua pindi wanapomuona na pia kuacha  imani potofu za kutumia viungo vyake kama njia ya kukuza biashara, kuondoa mikosi na matumizi mengine kama hayo.

Kwa mujibu wa utafiti huo, Kakakuona ana uzito usiozidi kilo 45, hubeba mimba kwa miezi mitano, huzaa mara moja kwa mwaka na mtoto mmoja, na chakula chake kikuu ni wadudu ambapo hula mchwa kwa asilimia 15 na siafu kwa asilimia 85.