Ded ubungo avutana na familia ya kada wa ccm

 

Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam

MKURUGENZI wa Manispaa ya Ubungo Jijini Dar Es Salaam Beatrice Dominic amejikuta akijiingiza katika mvutano mkubwa baina yake na familia ya Marehemu Said Mziwanda ya Goba kufuatia hatua ya wataalamu kitengo cha ardhi kutoka ofisi ya mkurugenzi Manispaa hiyo kuanza kuchimba eneo la shamba la familia ili kuanza ujenzi wa kituo cha afya bila kufuata taratibu

Hatua hiyo imekuja kufuatia mgogoro baina ya mkurugenzi wa Manispaa ya Ubungo na familia ya marehemu Said Mziwanda kugombea eneo hilo lenye ukubwa wa ekari 21 ambalo linafahamika kama Shamba la Mziwanda Tegeta A Goba lilianza kugombaniwa baada ya Manispaa ya Ubungo kufungua shauri la jinai namba 57/2021 dhidi ya msimamizi wa mirathi wa familia hiyo Salum Said wakidaiwa kuvamia eneo la serikali ya mtaa wa Tegeta A ambako walikuwa wanalima kilimo cha mihogo na Pamba miaka ya nyuma

Katika shauri hilo la jinai Hakimu aliomba vielelezo kutoka Manispaa vinavyoonesha uhalali wa umiliki lakini ofisi ya mkurugenzi haikuweza kuwasilisha kielelezo chochote na Hakimu kutoa ushindi kwa mlalamikiwa kuendelea kulitumia eneo hilo kwa kuwa mlalamikaji alikosa ushahidi kuthibitisha uhalali wa kulichukua shamba hilo 

Akizungumzia sakata hilo msimamizi wa mirathi ya familia ya Mziwanda Salumu Mziwanda ameiomba serikali ya Mama Samia kutenda haki kwa kuwa eneo lao ni shamba la asili walilorithi kutoka kwa marehemu Said Mziwanda aliyefika Goba miaka ya 1967

Salumu amesema inasikitisha sana Manispaa kutumia nguvu badala ya kukaa mezani kujadili endapo eneo hilo wanalitaka kutumia kwa matumizi ya Umma “angalia hali ilivyo mwandishi, ona makatapila yamezunguka kusawazisha eneo ambalo wanataka kujenga kituo cha afya wakati shauri hili linashughulikiwa na ofisi ya makamu wa Rais ambapo walitueleza tuwe na subira tukisubiri, lakini Leo wamekuja na migambo wanachimba eneo la shamba, namuomba mama Samia aingilie kati, tunamuomba waziri wa ardhi na makazi waje waangalie sisi wanyonge tunaonewa” alisema

Alipotafutwa mkurugenzi wa amanispaa ya Ubungo Beatrice Dominic kwa njia ya simu alisema yupo safarini anauguza mgonjwa na kukiri hafahamu kama kuna watumishi kutoka ofisi ya mkurugenzi wako shambani hapo “Naheshimu vyomba vya habari, naomba mtafute msaidizi wangu afisa ardhi ambaye atakupa majibu yote” alimaliza

Afisa Mipango Miji Fadhili Hussein amesema Manispaa ilipokea maagizo kutoka juu kulilinda eneo hilo na anashangaa kwanini kuna maafisa walifika kuanza kuchimba eneo hilo kwa ajili ya ujenzi wa Kituo cha afya “Hakuna kitu kama hicho ndugu mwandishi, sisi kazi yetu kwa sasa ni kulinda shamba hilo lisivamiwe na watu bila maelekezo ya serikali” alimaliza