El nino yatepetesha serengeti, wataalamu tanapa wakuna vichwa wakielekea unesco

Kamishna Mkuu wa Uhifadhi hifadhi ya Taifa Tanapa, Juma Kuji akitoa maelekezo kwa Msaidizi wa Uhifadhi, Mhandisi Mshauri, Daktari Richard Matolo ndani ya hifadhi ya Serengeti walipokuwa wakifanya ukaguzi wa barabara ndani ya hifadhi ambazo zimeharibiwa na mvua za El nini. 

Na Mwandishi Wetu, Serengeti 

MVUA za El Nino zinazoendelea kunyesha nchini na ambazo hazijapata kunyesha kwenye Hifahi ya Taifa ya Serengeti kwa takriban miaka 64, zimeitepetesha na kusababisha uharibifu wa miundombinu ya barabara na madaraja.

Tathmini ya wataalamu wa miundombinu ya barabara wa Mamlaka ya Hifadhi za Taifa (TANAPA), zimeonyesha kuwepo kwa athari kubwa kwenye barabara kuu nne zinazopita ndani ya hifadhi na pia zinazounganisha hifadhi na maeneo mengine ya nchi na sasa wanakusudia kuliandikia Shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu, Sayansi na Utamaduni kuomba kibali cha kufanya matengenezo. 

Kwa Mujibu wa Kamishna Msaidizi wa Uhifadhi, Mhandisi Mshauri, Daktari Richard Matolo, barabara zilizoharibika kwa kiwango kikubwa zinatumiwa na watalii, wahifadhi na magari yanayosafirisha abiria na mizigo.

“Barabara za hifadhini zilizoharibika sana ni barabara kuu nne; ya kwanza inatoka Golini kupitia Nabi hadi Soronera, yenye urefu wa kilomita 68, ya pili inatoka Soronera mpaka Dambaga, wilayani Magu, yenye urefu wa kilomita 121, ya tatu inatoka Soronera mpaka Ikoma Gate, yenye urefu wa kilometa 30 na ya nne inatoka Banagi kupitia Robo hadi Cleans Gate, yenye urefu wa kilomita 72,” alisema Kamishna Matolo,

Alisema barabara hizo zimeharibika kwa sababu hazitumiki kwa shughuli za uhifadhi pekee bali zinaunganisha hifdhi na maeneo ya nje hivyo zinatumiwa pia na magari ya usafirishaji ya umma yakiwemo mabasi na maroli.

Kamishna Matolo alisema, barabara hizo zinaunganisha hifadhi na maeneo muhimu ya kiuchumi yanayozunguka Hifadhi za Taifa.

Sambamba na barabara na madaraja, sehemu nyingine za hifadhi ambazo imezifikia Mwandishi Wetu wakati wa ukaguzi wa uliofanywa na maafisa wa juu wa TANAPA ni eneo kubwa la hifadhi kujaa maji.

Kamishana Matolo amelizungumzia hilo akieleza kuwa ni kwa sababu udongo wa hufadhini ni tifutifu na haujapata mvua kubwa ya kiwango cha mwaka huu tangu mwaka 1959.

Alisema ili kukabiliana na changamoto hiyo, Serikali ina mpango wa kujenga barabara bypass itakayopita kusini mwa Hifadhi ya Serengeti ambayo itatumiwa na magari makubwa ya kusafirisha mizigo na abiria na kwamba hilo litapunguza uharibifu wa barabara kuu za hifadhini.

Kamishna huyo alisema hivi sasa watalaamu wa TANAPA wanaendelea kutambua maeneo ya barabara yaliyoharibika na kuyafanyia ukaratabati wa dharura ili magari yaendelee kupita.

“Lengo la TANAPA ni kutengeneza barabara kuu nne za ndani ya hifadhi ili ziweze kupitika wakati wote na hili litafanyika baada ya mvua kupungua lakini mpango wa muda mrefu ni kuzitengeneza kwa kuziimarisha barabara hizo kwa kiwango cha kuweza kupitika wakati wote.

“Tunafikiria kutumia tabaka gumu kujenga barabara hizo, wenzetu wa Ngorongoro wameishafanya maandiko ya kitaalamu wakawasilisha UNESCO nao wakawapa kibali cha kuimarisha barabara yao kuu yenye urefu wa kilomita 83 kutokea Lango la Rodwale hadi Golini,” alisema Kamishna Matolo.

Akiendelea, alisema uendelezaji mkubwa wa maeneo ya Hifadhi ya Serengeti na Ngorongoro yanahitaji kibali cha UNESCO kwa sababu ni maeneo yanayotambulika na shirika hilo kama maeneo ya urithi wa dunia.

Akizungumzia daraja lililozua mjadala mitandaoni likidaiwa kuhatarisha maisha ya watalii, alisema daraja hilo halijaharibika bali lilijaa maji kutokana na wingi wa mvua zilizonyesha ambazo hifadhi hiyo haijawahi kuzipata.

Alisema kalvati zilizowekwa kwenye daraja hilo zilizibwa na kinyesi cha viboko na uchafu uliosombwa na maji kutoka sehemu mbalimbali za hifadhi hivyo maji yakawa yanapita juu ya barabaraba.

“Hayo ni mambo ya mtandaoni, kama daraja lingekuwa limekatika au halipitiki mbona sisi na wewe mwandishi tumepita? Daraja limejaa maji kwa sababu ya mvua inayonyesha. Kilichotokea baada ya maji kujaa watu waliokuwa upande ule walishindwa kufika upande ule mwingine kwa sababu ya kujaa maji na hili tunalifanyia kazi,” alisema Kamishna Matolo.

Alisema mpango wa TANAPA ni kujenga daraja litakalokuwa linapita juu ambalo litatumika wakati wa mvua kubwa kama zinazonyesha sasa ambapo daraja dogo la sasa litakuwa limefungwa na kuongeza kuwa wakati wa kiangazi madaraja yote mawili yatatumika.