Jiji la arusha kuupamba mji wake usiku kwa taa za kisasa

 Na Magesa Magesa, Arusha


HALMASHAURI ya Jiji la Arusha imesema kuwa imejipanga kung’arisha maeneo yote ya katikati ya mji  nyakati za usiku kwa kuweka taa  za kisasa na  tayari wametenga bajeti kwa ajili ya utekelezaji wa mradi huo.

Kaimu Mkurugenzi wa Jiji la Arusha,Hargeney Chitukulo aliyasema hayo jana alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake na kueleza kuwa lengo la mpango huo ni kuhahakikiskisha kunakuwa na mwanga haswa kwa suala zima la usalama.

“Kama mjuavyo Arusha ni mji wa kitalii kunapokuwa na giza kunawapa wakati mgumu watalii kutembea nyakati za usiku, hivyo mpango huu utasaidia watalii kutembea nyakati hizo pasipo na hofu yeyote kwa usalama wao pamaja na wakazi wa hapa”alisema

Chitukulo aliongeza kuwa katika kuhakikisha kuwa jiji linakuwa safi wakati wote halimashauri ya jiji pia imetenga fedha kwa ajili ya kuweka vifaa vya kuwekea taka(dustbin) katika maeneo mbalimbali hali ambayo itasaidia kuepusha wananchi kutupa taka nyepesi ovyo.

Kaimu mkurugenzi huyo wa jiji la Arusha alisema kuwa miradi yote hiyo miwili ambayo utekelezaji wake utaanza hivi karibuni unatarajia kutumia zaidi ya shilingi bilioni moja ambapo taa zitagharimu  milioni 400 na vifaa vya kuhifadhia taka milioni 700.

“Nitoe wito kwa wananchi wa jiji hili kuhakikisha kuwa wanalinda miundombinu ya miradi hii miwili ya taa na vifaa vya kuhifadhia taka nyepesi na kila ili itumike kwa muda mrefu na kila mmoja awe mlinzi wa mwenzake”alisisitiza.

Kadhalika alimpongeza Rais wa jamhuri ya muungano wa Tanzania,Samia Suluhu Hasan kwa kuipatia Halimashauri hiyo shilingi milioni 500 kwa ajili ya kujenga soko la wamachinga na kusema kuwa soko hilo litajengwa katika eneo la Bondeni City mjini hapa.</

span>

“Soko hilo litakuwa ni mkombozi mkubwa sana kwa wafanyabiashara kwani litakuwa kubwa na la kisasa na fedha hizo ni za kuanzia tu halmashauri itakuwa ikiendelea kutoa fedha kupitia vyanzo vyake vya ndani hatua kwa hatua hadi hapo litakapokamilika”alisema Chitukulo.