Mauaji ya kutisha shinyanga, auawa na kutobolewa macho

 

Na Mapuli Misalaba, Shinyanga

Kijana ambaye hajafahamika jina wala makazi yake, anaye kadiriwa kuwa na umri wa miaka (25-30), amekutwa ameuawa na kutobolewa macho, katika Ghuba la kuhifadhia uchafu la Ngokolo mitumbani Manispaa ya Shinyanga na watu wasiojulikana.

Mwenyekiti wa Mtaa wa Mwinamila katika eneo hilo la tukio Amir Athumani, amesema tukio hilo limetokea usiku wa kuamkia leo ambapo amesema baada ya kufika eneo la tukio majira ya saa moja asubuhi, ameukuta mwili wa kijana huyo akiwa ameuawa kinyama na kutobolewa macho, na watu ambao bado hawajafahamika.

” Tukio hili nila pili la watu kuuawa kwenye Ghuba hili la uchafu, akiwamo na mtoto mdogo kuuawa na kuweka ndani ya boksi, hivyo naomba wananchi kama wana migogoro, watafute ufumbuzi na kuacha kujichukulia sheria mkononi,” amesema Athumani.

Aidha Athumani amesema  watu mbalimbali wamefika kuuona mwili wa kijana huyo, lakini hakuna ambaye amemtambua, ambapo bado wanaendelea na jitihada na kutambua ndugu zake, ili wapatikane na kuupunzisha kwenye makazi yake ya milele.

Kwa upande wake Kamanda wa Jeshi la Polisi mkoani Shinyanga Kamishna msaidizi wa Polisi George Kyando, amethibitisha kutokea kwa tukio hilo, na kubainisha bado wanafanya upelelezi ili kubaini wauaji pamoja na chanzo chake.

Kamanda Kyando amesema katika eneo la tukio, Jeshi la Polisi wamekuta pembeni ya mwili wa marehemu kuna vyuma, ambavyo wanazani ndivyo vimetumika kufanyia mauaji, na kueleza kuwa Mwili wa marehemu umehifadhiwa kwenye chumba cha maiti katika Hospitali ya Rufani mkoani Shinyanga.