Mganga ajinyonga baada ya mkewe kuolewa na mwanaume mwingine

Polisi nchini Uganda wanachunguza kisa ambapo daktari wa kienyeji katika Wilaya ya Butaleja alijitoa uhai baada ya mke wake kuolewa na mwanamume mwingine.


Joseph Mwigo, mwenye umri wa miaka 38, anadaiwa kuwa na ugomvi wa kinyumbani na mke wake kabla ya kujizamisha kwenye bwawa la samaki la Ahmed Kambo Umoja siku ya Jumanne, Januari 24.

Kwa mujibu wa ripoti ya vyombo vya habari nchini humo, mke wake Mwigo alikuwa ameolewa na mmoja wa wakazi katika kijiji jirani jambo ambalo lilimfanya marehemu kunywa sumu mara ya kwanza.

Alikimbizwa katika Hospitali ya Busolwe mnamo Desemba 27, 2022, ambako alilazwa na baadaye aliruhusiwa kwenda nyumbani baada ya kupata nafuu.

Polisi waliwaambia waandishi wa habari kwamba Mwigo ambaye pia alipata ulemavu wa macho mwaka mmoja uliopita, amekuwa akitishia kujitoa uhai.

Jirani wake alifichua kuwa mganga huyo alikuwa akikumbwa na msongo wa mawazo tangu mke wake alipopata mwanamume mwingine.

Mabaki ya marehemu yaliopolewa kwenye bwawa mnamo Jumanne, Januari 24, na kupelekwa katika Chumba cha kuhifadhi maiti cha Mbale City kwa uchunguzi wa maiti.

Chanzo: Tuko News