Rais samia aiagiza tanroads kudhibiti waharibifu wa barabara

 Na Mwandishi Wetu, Dar es salaam.

Rais wa Samia Suluhu Hassan amezindua awamu ya pili ya ujenzi wa barabara ya mwendo kasi katika Jiji la Dar es salaam na kuwataka wasimamizi wa mradi huo wakala wa barabara nchini (TANROADS),kufanya kazi kwa bidii ili kumaliza kazi hiyo kwa wakati.

Rais Samia pia ameagiza kufanyika kwa doria kufuatia kuwepo kwa watu ambao wamekuwa wakivamia maeneo ya hifadhi ya ujenzi wa  barabara na kujenga vibanda vya biashara bila kujali maelekezo yanayotolewa na hivyo kuhatarisha maisha yao na watumiaji wengine.

“kuna vitendo vinafanywa na baadhi ya watumiaji wa barabara, kama vile kuzidisha uzito wa magari, kumwaga mafuta barabarani, kuziba mifereji ya maji,uegeshaji holela wa magari ambavyo vinasababisha kuharibu mazingira kwa ujumla, naagiza kufanyike doria kuzuia vitendo hivi,” alisema Rais.

Mtendaji Mkuu wa Wakala ya Barabara Tanzania (TANROADS), Mhandisi Rogatus Mativila amesema ujenzi wa mradi huo unahusisha ujenzi wa barabara zenye urefu wa km20.3.

“Ujenzi wa Mradi huu unahusisha ujenzi wa miundombinu ya barabara zenye urefu wa Kilometa 20.3, ikiwemo ya Kilwa kutoka Makutano ya Barabara ya Bandari hadi Mbagala yenye urefu wa kilometa 11.3”.

“Barabara ya Bandari hadi Gerezani, Kariakoo yenye urefu wa kilometa 4, barabara ya Chang’ombe kutoka makutano ya barabara ya Nyerere hadi Mgulani yenye urefu wa Kilometa 2.8 na barabara ya Kawawa inayotoka Magomeni hadi Nyerere yenye urefu wa Kilometa 3.5”.

Mhandisi Mativila ametaja barabara nyingine kuwa ni pamoja na barabara ya Sokoine kutoka Gerezani hadi kati kati ya Jiji yenye urefu wa kilometa 1.3″ alisema.

Amesema mradi huo pia unahusisha ujenzi wa madaraja ya juu, Karakana na Vituo vya Mabasi ambamo magari ya mwendo kasi yatasimamia kupakia abiria .