Serikali imeombwa kuweka utaratibu maalumu wa kuweza kuwatembelea wakulima mbalimbali

Serikali imeombwa kuweka utaratibu maalumu wa kuweza kuwatembelea wakulima mbalimbali wa mazao ya miti ambao wanafanya kilimo cha miti na misitu ili waweze kuboresha zaidi kilimo hicho ambacho kina tija kubwa sana kwa jamii 

Hayo  yameelezwa na Nolasco Nkawe ambaye ni  mwanaharakati wa mazingira ambaye pia ni mkulima wa miti mbalimbali kutoka mkoa wa Arusha. 

Nkawe alisema kuwa kwa Sasa Wanaharakati wa mazingira huwa wananunua miti kutoka Katika vitalu vya miti bila kuhamasishwa na mtu yeyote kutoka Serikalini 

Alifafanua kuwa wakulima wa miti wanapanda miti na kuitunza wakiwa wenyewe bila mtu yeyote ya halmshauri au wizara kuwatembelea lakini wanapofikia kukata miti maafisa  wa Serikali hujitokeza 

“Ile nguvu ambayo maafisa hawa wanakuwa nayo kwenye kukata miti inatakiwa nguvu hiyo hiyo iweze kuhamasisha na kutatua kero za Wana harakati wa mazingira kama kweli tunatamani ongezeko la miti katika jamii zetu”alisisitiza 

Katika hatua nyingine alisema kuwa Ni muhimu sasa kwa Serikali kuangalia upya namna ya kuhamasisha jamii iweze kupanda miti kuanzia kwa watoto jambo ambalo litawafanya wayapende na kuyathamini mazingira

“Tukianzisha uhamasishaji wa upandaji wa miti kuanzia kwa watoto basi ule ukijani ambao unatokana na miti utarudi tena na pia hawa watoto wataweza kujua kuwa faida na umuhimu wake”aliongeza hivyo 

Pia alisema kuwa ili kuifadhi na kulinda rasilimali misitu na miti tayari mpaka Sasa ameshapanda miti zaidi ya elfu 20 ambapo miti hiyo hutumika kwa matumizi mbalimbali ikiwemo nguzo za umeme.

Alihitimisha kwa kusema kuwa miti Ni uhai na ili kizazi kijacho kiweze kuikuta nchi ikiwa na rasilimali hasa zile za asili Ni muhimu sana suala la utunzaji wa miti likapewa kipaumbele.