Taasisi za fedha arusha zatakiwa kuzingatia maadili

  Magesa Magesa, Arusha

MKURUGENZI  wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT) Tawi la Arusha,Charles Yamo amewataka watoa huduma katika Taasisi za kifedha Mkoani hapa kuhakikisha wanatoa huduma zao kwa kuzingatia maadili na weledi.

Ameyasema hayo leo Juni 1, 2022 jijini hapa alipokuwa akifungua semina ya  Bodi ya Taifa ya wahasibu na wakaguzi(NBAA) unaoendelea mjini hapa na kuwataka kuhakikisha pia wanazingatia misingi ya taaluma zao.

“Suala la nidhamu na maadili imekuwa ni changamoto kwa baadhi ya watumishi katika taasisi za kifedha hivyo natoa wito kwa wale wote wanafanya kazi zao kinyume na maadili na weledi kuacha mara moja kwani watachukulia hatua kali za kisheria”alisisitiza.

Yamo amewataka watumishi hao kuhakikisha kuwa wanatoa taarifa sahihi na za ukweli kwa wakati kwa wateja wao ili waendelee kuwa na imani nao ikiwa ni pamoja na kuzingatia yale yote watakayofundishwa katika semina hiyo na kwenda kuyafanyia kazi kwa vitendo.

Kwa upande wake Mtendaji Mkuu wa NBAA ambao ndio waandaji wa semina hiyo kwa kushirikiana na Benki Kuu(BoT)Pius Maneno alisema kuwa semina hiyo ya siku tatu inawashirikisha wahasibu,wato huduma za kifedha,kodi na bima na kwamba unawashirikisha zaidi ya washiriki 400 kutoka maeneo mbalimbali nchini.

Aliongeza kuwa lengo la semina hiyo ni kuweza kuwapa mafunzo washiriki juu ya utoaji huduma bora kwa wateja wao ikiwamo kukumbushana majukumu  ya taaluma ya uhasibu na benki.

“Pia tunawahimiza matumizi ya Teknolajia ya habari na Mawasiliano(TEHAMA) katika kufanya kazi zao ili kuendana na kasi ya ukuaji wa tekolojia hapa nchini na ulimwenguni kwa ujumla.”alisema mtendaji mkuu huyo wa NBAA.

Kwa upande wao baadhi ya washiriki wa semina hiyo waliipongeza NBAA na BoT kwa kuandaa mafunzo na kuahidi kwenda kuyafanyia kazi kikamilifui kiwa ni pamoja na kutoa elimu waliyoipata hapo kwa wengine.