Vijana toka mazingira magumu mufindi wapewa elimu ya ujasiliamali na mradi wa yam

 

Vijana wanaotoka kwenye mazingira magumu kata tatu za wilaya ya Mufindi wakiwa kwenye mafunzo ya ujasiliamali

ZAIDI ya  vijana  80 wanaotoka katika mazingira  magumu kata tatu za Igoda , Luhunga  na Mdabulo  wilaya ya  Mufindi  mkoani  Iringa  wameanza  kupatiwa  mafunzo maalumu  ya uanzishaji miradi ya kiuchumi itakayowawezesha  kuendesha maisha yao na  kusaidia familia zao.

Mafunzo hayo ya siku 10 yameanza jana katika  ukumbi  wa Yatima kijiji  cha Igoda  wilaya ya  Mufindi   kwa  kushirikiasha vijana  hao  ambao baadhi yao  ni  wale  ambao wamekatisha masomo kwa  changamoto  mbali mbali kimaisha  ikiwa  ni pamoja na mabinti waliokatisha  kwa  ujauzito .

Mkufunzi  wa mafunzo hayo John Kalolo kutoka  shirika lisilo la kiserikali la RLABS -Tanzania  alisema  kuwa  mafunzo hayo maalum ni ya  kuwajengea  uwezo  wa katika  nyanja ya  ujasiliamali   yatawezesha  vijana  hao  kuweza  kuondokana na  fikra mgando ambazo baadhi yao   wamekuwa nazo kuwa  ili  uwe  mjasiliamali  ni lazima  kuwa na   fedha mkononi  wakati unaweza  kuwa mjasiliamali bila ya kuanza  na  mtaji  wa  fedha .

“Maeneo mengi ya  vijijini kuna  fursa  nyingi za  kufanya ambazo kimsingi  ni  moja kati ya  mtaji  mkubwa  kwa  mtu ambae  anatamani  kuwa mjasiliamali hivyo iwapo  wahusika  wataondokana na fikra mgando  za kutegemea fedha  wanaweza kupiga hatua katika maisha” alisema

Kuwa  ili  vijana hao  waweze  kuondokana dhana  hiyo  potofu ni lazima  kwanza  kujitambua na kujiamini kabla ya   kuanza  shughuli ya  ujasilimali  ambayo anahitaji kuifanya  na baada ya kuanza  ndipo  wanaweza  kuanza mchakato wa pili  wa  kuomba mikopo ya kuboresha shughuli  husika ya  ujasiliamali.

Hata  hivyo  alisema  kupitia ardhi walizonazo vijijini  ziwe  za familia ama  zao binafsi wanaweza  kubuni miradi ya  kiuchumi ambayo miradi  hiyo haihitaji  mtaji mkubwa wa  fedha  zaidi ya  kuhitaji nguvu kazi ya mkono.

Kalolo  alisema mfano ujasiliamali  wa  ususi kwa mabinti ni  ujasiliamali  ambao  mtu anaweza  kuanza kwa ubunifu  usio tegemea  fedha  na baada ya  kuanza ndipo   wanaweza  kuboresha kwa  kutafuta eneo litakalohitaji fedha  za kuboresha zaidi.

Akizungumzi faida ya mafunzo  haya meneja  wa mradi  wa Youth Agency Mufindi (YAM) Zilipa alisema lengo la mafunzo hayo ni   kuwawezesha  vijana  zaidi ya  770 wakiwemo  watoto  150 yatima  kutoka   kata   hizo tatu   ambazo  zote  zitaunganishwa na  vijiji  16  za  mradi  huo .

Alisema  mradi  huo wa  YAM ni wa miaka minne toka mwaka 2021/2024 umefadhiliwa na    serikali  ya Filands  chini ya taasisi yake ya Diaconess   kwa  ushirikiano  wa  serikali ya Tanzania chini ya Halmashauri ya  wilaya  ya Mufindi na taasisi ya  Foxes Community and Wild Life Conservation.                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                                      

Mgeni  alisema  baada ya mafunzo hayo  kutolewa kwa  walengwa  watawezeshwa  mitaji ya  kuendeshea miradi  ambayo watakuwa wamechangua  kuifanya kwa  kuwaongezea  nguvu ya  kuiboresha  zaidi.

Wilaya ya Mufindi  ni  moja kati ya  wilaya  tatu  za  mikoa  wa Iringa ambazo   zimekuwa na changamoto ya    vijana na  watoto  wanaoishi katika mazingira magumu na kupitia   serikali na  wadau mbali mbali wa maendelea  wameendelea  kuwawezesha   vijana  hao  ili kuanzisha  miradi ya kiuchumi inayowafanya  kupiga  hatua za  kimaendeleo .