Mahakama kuu yakubali act- wazalendo kujiunga kwenye kesi kuhusu ukomo wa urais



Mahakama
Kuu Kanda ya Dar es Salaam imekubali ombi la Chama cha ACT-Wazalendo
kujiunga kama washtakiwa kwenye kesi ya kikatiba iliyofunguliwa na
Dezydelius Mgoya, maarufu kama Mkulima, kuhusu ukomo wa urais.


Uamuzi
huo ulitolewa jana na Jaji Dk. Benhaj Masoud baada ya kusikiliza maombi
ya ACT-Wazalendo kujiunga na kesi hiyo kwa sababu wana maslahi nayo.

Wakili
wa ACT-Wazalendo, Jebra Kambole, alidai kuwa mteja wake ameomba
kujiunga kwa sababu ni chama kilichosajiliwa na kimeshiriki katika
uchaguzi.

Pia alidai kuwa chama hicho kina wanachama Tanzania Bara na Visiwani Zanzibar kwa mujibu wa matakwa ya kisheria na kikatiba.

Mgoya
alifungua kesi hiyo chini ya kifungu cha 4 cha sheria ya utekelezaji
haki na wajibu, sura ya 3 ya mwaka 1994 chini ya Ibara ya 30(3) ya
Katiba ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977.

Kwa
mujibu wa hati ya madai ya kesi hiyo, Mgoya anahoji Ibara ya 40(20) ya
Katiba ambayo imeweka ukomo wa mihula miwili tu ya miaka mitano mitano
ya uongozi katika nafasi hiyo ya urais.

Hivyo
anaiomba mahakama hiyo itoe tamko na tafsiri ya maana sahihi na athari
za masharti ya ibara hiyo.Pia anaiomba mahakama itoe tafsiri ya maana
dhahiri ya masharti ya Ibara ya 42(2) ya Katiba kwa kuhusianisha na
masharti ya Ibara za 13, 21 na 22 za Katiba hiyo.

Kadhalika, Mgoya anaiomba mahakama itoe tafsiri ya maana ya Ibara hiyo ya 40(2) kwa kuhusianisha na Ibara ya 39 ya Katiba.

Credit:Nipasahe