Msalaba mwekundu laonya kuhusu habari za uongo za chanjo ya covid-19

Na Mwandishi wetu, APC BLOG

Mkuu wa Shirika la
Msalaba Mwekundu, Francesco Rocca amesema kwamba taarifa zisizo sahihi kuhusu
chanjo ya COVID-19, zinaweza kusababisha ”janga la pili.”

Rocca,
rais wa Shirikisho la Kimataifa la Msalaba Mwekundu na Hilali Nyekundu,
ameuambia mkutano uliofanyika kwa njia ya video kwamba mapambano ya virusi vya
corona ni kulishinda janga jengine linalofanana la kukosekana kwa uaminifu.
Amezitaka serikali na taasisi kupambana kikamilifu na ”taarifa za uwongo”
kuhusu chanjo ya COVID-19, ambalo limekuwa ”janga la pili.” Amehimiza
kuijenga jamii yenye kuaminiana ulimwenguni na kuelezea kuhusu umuhimu mkubwa
wa kuwachanja watu.

Rocca
ametolea mfano utafiti wa Chuo Kikuu cha Johns Hopkins uliofanywa katika nchi
67 ambao umegundua kutokukubalika kwa chanjo kwenye nchi nyingi kuanzia Julai
hadi Oktoba mwaka huu. Katika robo ya nchi hizo, watu waliikubali chanjo hiyo
chini ya asilimia 50.

Amesema Japan uaminifu ulishuka
kutoka asilimia 70 hadi 50 na Ufaransa ulipungua kutoka asilimia 51 hadi 38.

Amesisitiza
kuhusu ukosefu wa uaminifu sio ”hali ya nchi za Magharibi,” akitolea mfano wa
utafiti wa shirikisho uliofanyika hivi karibuni kwenye nchi nane za Afrika. Utafiti
kwenye nchi za, Kongo, Cameroon, Gabon, Zimbabwe, Sierra Leone, Rwanda, Lesotho
na Kenya umeonesha kushuka kwa kasi mtazamo kuhusu hatari ya maambukizi ya
COVID-19.

Idadi
kubwa ya watu wameonesha kuwa virusi vya corona haviwaathiri vijana wa Afrika
na kwamba ugonjwa huo haupo kwa sasa. Amesema kwenye nchi kadhaa za Afrika,
wameshuhudia imani iliyojengekea kwamba nchi za kigeni zinaitumia Afrika kama
sehemu ya kufanya majaribio ya chanjo.

Wakati
hayo yakijiri mshauri wa Rais wa Marekani Donald Trump, kuhusu virusi vya
corona, Scott Atlas amejiuzulu. Ametangaza uamuzi wake wa kujiuzulu jana jioni.
Atlas ambaye hana uzoefu kuhusu afya ya jamii au magonjwa ya kuambukiza,
alizusha mjadala wenye utata kutokana na matamshi yake kupinga uvaaji wa barakoa
na kuhusu masuala mengine ya kudhibiti virusi vya corona.

 

Maambukizi
Ujerumani

 

Nchini
Ujerumani, takwimu zilizotolewa Jumanne na Taasisi ya Kudhibiti Magonjwa ya
Kuambukiza, Robert Koch zinaonesha kuwa visa vya COVID-19 vimeongezeka hadi
13,604 na vifo 388. Aidha serikali ya Ujerumani imekubali kuanzissha maeneo 19
kwa ajili ya kuhifadhi vifaa vya matibabu ili kuzuia uhaba wa barakoa na vifaa
vingine vya kujikinga, tatizo linaloikumba dunia tangu kuzuka kwa janga la
virusi vya corona.

Nalo
Shirika la Umoja wa Mataifa la uratibu wa misaada ya kiutu, OCHA, limesema leo
kuwa janga la COVID-19 limechochea kuongezeka kwa asilimia 40 ya idadi ya watu
wanaohitaji msaada wa kiutu duniani. Shirika hilo limeomba msaada wa takriban
dola bilioni 35 kwa ajili ya kuwasaidia watu milioni 235 watakaohitaji msaada
mwaka ujao wa 2021.

Wakati
huo huo, imeripotiwa kuwa kiongozi wa Korea Kaskazini, Kim Jong Un na familia
yake wamepewa chanjo ya majaribio ya virusi vya corona iliyotengenezwa China.
Taarifa hizo ni kwa mujibu wa mchambuzi wa Marekani kuhusu masuala ya Korea
Kaskazini, Harry Kazianis, ambaye amevinukuu vyanzo viwili vya kiitelijensia
vya Japan