Waziri ndaki awataka wananchi kushirikiana katika suala la kudhibiti uvuvi haramu

 

Waziri
wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Mashimba Ndaki akizungumza na Viongozi wa
Serikali wa Kanda ya Ziwa Victoria kuhusu ulinzi na usimamizi shirikishi
wa rasilimali za uvuvi katika ukumbi wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Mwanza




Na Elibariki Mafole, MWANZA


WANANCHI
wametakiwa kushirikiana katika suala la kudhibiti uvuvi haramu Ziwa
Victoria ili kuendelea kunufaika na rasilimali za uvuvi.


Hayo
yalisemwa na Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mashimba Ndaki, katika kikao cha
wadau wa Uvuvi kanda ya Ziwa kilichojadili kuhusu ulinzi na usimamizi
wa rasilimali za Uvuvi na kusema suala la udhibiti wa uvuvi haramu
katika mwambao huo ni la kila mmoja.


Mashimba
alisema suala la ulinzi wa rasilimali zilizopo ziwani ni jukumu la kila
mmoja katika ngazi zote kuanzia kitongoji mpaka wilaya hadi wizarani
na si jukumu la askari kudhibiti uvuvi haramu.



“Ikiwa uvuvi haramu tutaukumbatia wenyewe mtajiangamiza wenyewe, ninyi
mnaofaidika na ziwa mpo, na athari mnaiona kwanini waje maaskari kutoka
Dodoma au sehemu nyingine kuja kufanya msako kwenu, ndugu zangu naomba
tushirikiane wote, ngazi ya Kitongoji, Kijiji, Kata wote hili ni jukumu
letu suala la uvuvi haramu halikubaliki” alisema Ndaki



Mashimba alisema ipo dhana inazungumzwa kuwa uvuvi haramu ni dhana tu
inayojengwa na wataalamu na serikali na kuna dhana nyingine kuwa samaki
wapo tu ziwani na kuongeza kuwa ikiwa uvuvi haramu tutaukumbatia
tutajiangamiza wenyewe


“Kuna
dhana kuwa uvuvi haramu ni dhana tu inayojengwa nawataalam na serikali ,
kwamba uvuvi haramu hamna, na dhana hiyo inasema kuwa samaki wapo ziwa
litaenda wapi, lakini ninyi wenyewe ni mashahidi, kuna wakati mmeanza
kulia ninyi wenyewe kwamba samaki hawapo, mpaka sasa upungufu upo sasa
kwanini isiwaume ninyi imuume zaidi waziri au Katibu Mkuu wa Uvuvi
ambaye nyumbani kwao ni Mtwara bahari pana kuliko ziwa letu, kwanini
lisituume sisi,” alisema Ndaki.


Mwenyekiti
wa kikundi cha usimamizi shirikishi wa rasilimali za uvuvi (BMU) Wilaya
ya Rorya Stephano Mchoye alisema halmashauri ishirikiane na vikundi
hivyo ili kudhibiti uvuvi haramu kwa manufaa ya vizazi vilivyopo na
vizazi vijavyo.


Ulinzi
shirikishi katika ziwa letu haujaanza leo, ninaomba Wizara iangalie
zana hizi zinazotumika tika uvuvi haramu zinatoka wapi dawa ya hiyo
ikishapatikana naamini uvuvi haramu Tanzania hautapatikana.


Kwa
upande wake Nadhil Sadick msambazaji wa mazao ya samaki nje ya nchi
aliomba serikali kuangalia tozo mbalimbali wanazotozwa pasipokuangalia
madhara yake kwa wanaotoza pamoja na wale wanaotozwa.


Mashimba
amewaagiza halmashauri pamoja na mabaraza ya madiwani kuangalia upya
tozo wanazotoza katika mialo na katika rasilimali mbalimbali za uvuvi
ili kuwapunguzia mzigo wavuvi.


“Niombe
halmashauri pamoja na mabaraza yenu ya madiwani hebu kaangalieni upya
tozo mnazowatoza kwenye mialo na mazao mbalimbali ya uvuvi, mkaangalie
upya tuone tutakapowapunguzia, tuwapunguzie mzigo kwenye hayo maeneo
tunayotoka,” alisema Mhe. Ndaki.


“Mimi
ni shahidi nimeenda kule Geita tozo za kwetu ngazi ya wizara kwa upande
wa dagaa ni mbili tu royality na leseni, lakini zipo tozo 8 ambazo
halmashauri inatoza, jumla tozo 10 anatozwa mtu mmoja halmashauri
tuangalie pia ustawi wa watu wetu, anaondoka na nini kwenye hicho
tunachotaka kumtoza vinginevyo mtapunguza mapato yeye ninyi wenyewe,”
alisema Mhe. Ndaki.