Bodi ya nafaka na mazao mchanganyiko yafufua kiwanda cha nmc arusha, kuanza uzalishaji

Na Seif Mangwangi, APC BLOG, ARUSHA

WAKULIMA wa mikoa ya Kanda ya Kaskazini wanatarajiwa kuondokana na adha ya masoko ya
kuuzia mazao yao hususani mahindi na ngano kufuatia kiwanda cha CPB kilichopo jijini hapa
kuanza uzalishaji hivi karibuni.

Akizungumza kiwandani hapo leo, Meneja Mwendeshaji wa kiwanda hicho, Kulwa Rwegasira
amesema CPB ambayo zamani ilijulikana kama ‘Monaban’ inatarajia kuanza kununua mazao ya
wakulima wa kanda ya Kaskazini na kuzalisha bidhaa mpya ya unga wa dona utakaojulikana kwa
jina la ‘Dona bora’.

Kiwanda hicho cha CPB kilichokuwa kikiendeshwa na mwekezaji, hivi sasa kinaendeshwa na
Serikali kupitia bodi ya nafaka na mazao mchanganyiko baada ya Serikali kukichukua kwa kile
kinachodaiwa mwekezaji kushindwa kulipa kodi ya pango.

Rwegasira anasema kiwanda hicho kitakuwa kikizalisha aina hizo za unga kwa kutumia vigezo
vya ubora wa kimataifa kwa kuwa mbali ya kusambazwa nchini pia utasambazwa kimataifa
ikiwemo nchini Kenya.

Anasema pia kiwanda hicho kiko kwenye matengenezo mbalimbali katika baadhi ya mashine
zake ili kiweze kuzalisha unga wa ngano kwaajili ya kutengenezea bidhaa tofauti hususani
vitafunwa.

“Mbali ya kuzalisha dona bora pia tutaanza kuzalisha unga wa ngano ambao na wenyewe
utakuwa unga bora tofauti na unga mwingine, lengo letu ni kuhakikisha mwananchi anapata
bidhaa yenye ubora wa hali ya juu,”anasema.

Rwegasira anasema CPB pia inatoa huduma za mizani, kusafisha mazao ya wafanyabiashara na
wakulima kwa bei nafuu, kukausha mahindi yanayokosa soko kutokana na kuwa na
unyevunyevu, pamoja na kukodishia wafanyabiashara maghala ya kuhifadhia mazao.
Kwa upande wao maafisa udhibiti ubora kiwandani hapo Abdallah Dengedu na Jonathan
Lunyemela wanasema wamejipanga kuzalisha bidhaa zenye ubora wa hali ya juu na na bei
nafuu ili kuleta tofauti katika soko.

Afisa mdhibiti ubora wa kiwanda cha CPB Jonathan Lukenyela akieleza namna ambavyo uzalishaji utafanyika katika kiwanda hicho pindi watakapoanza uzalishaji, nyuma ni mashine za kisasa zitakazotumika.

Meneja wa kiwanda cha CPB Arusha, Kulwa Rwegasira akielezea ujio wa kiwanda

kipya cha CPB kwa lengo la kuwanyanyua wakulima kwa kununua bidhaa zao pamoja na
kuzalisha bidhaa bora kwa walaji.

Afisa udhibiti ubora uzalishaji wa kiwanda cha CPB Ramadhan Dendegu akielezea waandishi wa habari ubora wa mashine za kiwanda hicho katika kudhibiti ubora wa bidhaa zitakazoanza kuzalishwa hivi karibuni pamoja na mifugo itakayotumika kuhakikisha ubora unakuwepo.