Teknolojia ya nyuklia mkombozi mpya kwa wakulima tanzania

Simon Mdoe Mtafiti mwandamizi wa teknolojia ya Nyuklia akiwa katika viwanja vya maonyesho ya nanenane Kanda ya kaskazini Themi Njiro Mkoani Arusha.

Mtafiti Mwandamizi wa teknolojia ya Nyuklia Simon Mdoe akimpatia Gadiel Kitomari, elimu ya teknolojia ya nyuklia katika kilimo alipotembembelea banda hilo katika viwanja vya maonyesho ya nanenane Kanda ya kaskazini Themi Njiro Mkoani Arusha

Peter Ngamilo 

Mkuu wa kitengo cha Mawasiliano wa taaasisi ya TAEC, Peter Ngamilo akimpatia mteja elimu ya teknolojia ya nyuklia katika kilimo mteja Gadiel Kitomari alipotembembelea banda hilo katika viwanja vya maonyesho ya nanenane Kanda ya kaskazini Themi Njiro Mkoani Arusha

Na Vero Ignatus,  APC BLOG, ARUSHA 

TUME ya Nguvu za Atomic Tanzania (TAEC) imefanikiwa kupata matokeo chanya ya utafiti wa mbegu ya mpunga ya Super Bc kwa kutumia teknolojia ya mionzi ya kununurisha vinasaba (viasili)vya mbegu hizo na kupelekea mavuno mengi zaidi visiwani Zanzibar.

Akizungumza na waandishi wa habari kwenye maonyesho ya nane nane kanda ya kaskazini  Simon Mdoe Mtafiti Mwandamizi wa Teknolojia ya Nyuklia,amesema utafiti huo ulioanza 2009 umefanikisha matokeo chanya mara saba zaidi kwa mavuno ya mbegu ya mpunga ya Super Bc huko visiwani Zanzibar ikilinganishwa na awali.


Amesema TAEC 
kwa kushirikiana na shirika la mbegu la Zanzibar, ZARI pamoja na chuo cha kilimo Sokoine (SUA)  ilianza utafiti wa mbegu hiyo ambapo walinunurisha kupitisha mionzi kitaalamu kwenye mbegu) ambayo ilibadilisha viasili (vinasaba) na kuwa bora zaidi kuweza kuzalisha mara saba ya mazao yaliyokuwa yakizalishwa awali.

“Utafiti wetu tulichukua mbegu za mmea wa mpunga na kupitisha miale ya nyuklia kwa hatua sita, huku kila hatua moja tukihamishia mbegu shambani na kupata matokeo tofauti, mara ya mwisho tulipata matokeo mazuri zaidi kuliko hatua nyingine tano na kugundua kuwa na mavuno yamefikia mara saba ya kawaida ya mbegu hizo kama mkulima anavuna magunia 19 kama ambavyo imezoeleka kwa mbegu za zamani na alipotumia mbegu zetu alipata gunia 80 za mpunguza”, anasema.

Mtafiti huyo amesema baada ya matokeo ya utafiti walishirikisha mashirika ambayo pia yalialika maduka ya mbegu visiwani Zanzibar na kuwapelekea wakulima ambao walipata matokeo  hayohayo mazuri mara saba zaidi tofauti na awali kabla ya utafiti.

Mdoe amesema pia matokeo mengine ya utafiti na kuboreshwa kwa mbegu kupitia mionzi ya nuklia yamebaini kuongezekana kwa ladha ya mchele uliotokana na mpunga wa Super Bc, pamoja na harufu nzuri kwa walaji.

“Pia matokeo ya tafiti yameonyesha mbegu hiyo kutoshambuliwa na wadudu wakati wa kuota na ukuaji wake”anasisitiza Mdoe.

Mtafiti huyo anasema TAEC kwa kushirikiana na Chuo cha kilimo cha Sokoine (SUA) wanaendelea na utafiti ili kununurisha mbegu nyingine za mpunga, zaidi ya Super Bc kwa kuzingatia hali ya hewa na maeneo tofauti ya Nchi na aina ya udongo ili kupata tija itokanayo na mavuno mengi kwa ustawi wa Uchumi wa Nchi.

Mdoe amesema utafiti wa kununurisha mbegu hizo  unafanyika kwenye kituo cha utafiti cha Ilonga Mkoani Morogoro na katika kituo cha Mati kilichopo eneo la Uyole Jijini Mbeya.

Tafiti nyingine kama hizo za mbegu za Mahindi na shairi zinazofanyika katika Kituo cha utafiti wa mbegu za Kilimo cha SELIAN, Arusha ambazo ununurishaji umeshafanyika na tayari mbegu hizo ziko kwenye hatua za mpando wa awali ambapo hatua yenye ubora wa juu utakapofikia tamati, zitasambazwa kupitia njia zilizofanyika Zanzibar kwa wakulima ili kuongeza mavuno na kukuza uchumi wa wakulima na Taifa kwa pamoja.

Amesema TAEC/(TAHA)kwa pamoja wako kwenye upembuzi yakinifu ili kuona namna ya kununurisha mboga mboga,matunda na maua ili kuhifadhika kwa muda mrefu na unaofaa pindi bidhaa inapokuwa sokoni kwa muda ili isiharibike kwa urahisi kwani uzoefu unaonyesha asilimia 40 ya matunda na mboga ,boga huharibika kwa kuoza kutokana kukosa teknolojia kama hiyo ya mionzi.

Amesema tafiti nyingine zinafanyika kwenye mbegu za wanyama kama N’gombe kwa njia ya uhamilishaji kwa kushirikiana na Tasisi ya mifugo ya uhamilishaji iliyopo Usa ya (NIC) ili kupata mifugo bora inayokidhi viwango vya ndani na nje kwa nyama bora.

Mkuu wa kitengo cha Mawasiliano TAEC  Peter Ngamilo amesema shirika hilo lina matarajio ya kuwa na mtambo wa kuzalisha vyanzo vya mionzi (Linear Acceletor)vinavyotumika kwenye matibabu, viwanda,kilimo na utafiti (Radioisotopes)


Anasema TAEC pia ina matarajio ya kuanzisha mradi wenye kutumia teknolojia ya nuklia katika kufanya tafiti mbalimbali (Nuclear Research Reactor)Zenye manufaa kwa Nchi ambapo Mtambo huo utaiwezesha Tanzania kuwa na viwanda vya madawa ya tiba ya saratani pamoja na kutumika kama nyenzo ya kufundishia katika taasisi za elimu ya juu na utafiti.

Tume ya nguvu ya Atomiki (Tanzania Atomic Energy Commission)ilianzishwa kwa  sheria ya Bunge no 7 ya Mwaka 2003, awali ilikuwa ikijulikana kama Tume ya taifa ya mionzi iliyoanzisha kwa sheria ya bunge no 5 Mwaka 1983 ambapo ina majukumu ya kuthibiti matumizi ya mionzi salama Nchini, kuhamasisha na kuendeleza matumizi salama ya Teknolojia ya Nyuklia  na kufanya utafiti.