Kesi kuhusu kuminya uhuru wa habari yaanza kusikilizwa

Kesi kuhusu kuminya uhuru wa habari yaanza kusikilizwa 

Sheria mpya ya vyombo vya habari nchini Tanzania ambayo ilipitishwa na rais wa nchi hiyo mnamo Novemba 2016, imeanza kusikilizwa rasmi leo katika mahakama ya Afrika Mashariki huko, Arusha, Kaskazini mwa Tanzania.
Kesi hiyo ilifunguliwa mwezi Januari 2017 na wanaharakati pamoja na wataalamu katika tasnia hio ya habari, wakiwa wanaamini kwamba sheria hio inakiuka mkataba wa Afrika Mashariki kwa kuminya uhuru wa habari na uhuru wa watu kujieleza katika nchi hio.
Madai ambayo wameyaainisha na wanaona kuwa sheria hiyo imekeuka ni kwa jinsi ambavyo Waziri amepewa mamlaka ya kuvifungia vyombo vya habari na kuwepo kwa ugumu kwa wageni kupata vibali vya kuja kuandika taarifa zao nchini humo.
Mkataba wa Afrika mashariki unataka kila nchi lazima ikuze demokrasia na uhuru wa kujieleza.Ingawa wanaamini kuwa hakuna uhuru ambao hauna mipaka lakini sheria hii inafanya uhuru usiwepo.
Aidha baraza la habari nchini Tanzania na wanaharakati wa haki za binadamu wanasema sheria mpya ya habari imetoa vifungu vinavyokandamiza tasnia hiyo ya habari katika kutoa taarifa.
Kesi hiyo imeanza kusikilizwa rasmi kwa njia ya maandishi kwa sasa ili kiini cha mgogoro uweze kupatikana.

Wadau wa habari walidahi kuwa walitoa maoni yao wakati sheria hiyo ikiwa inaandaliwa lakini wanadhani kuwa ushauri wao haukuzingatiwa hivyo inabidi irekebishwe tena.