Mtu mfupi zaidi duniani afariki dunia

Khagendra Thapa Magar enzi za uhai wake

Mtu mfupi zaidi duniani ambaye anaweza kutembea kama ilivyothibitishwa
na kitabu cha rekodi za dunia cha Guiness amefariki hospitalini Nepal
akiwa na umri wa miaka 27.
Khagendra Thapa Magar, kutoka wilaya ya Baglung alikuwa na urefu wa sentimita 67.08cm sawa na futi mbili na nchi 4..
Nduguye aliambia chombo cha habari cha AFP kwamba alifariki siku ya Ijumaa baada ya kuugua homa ya mapafu.
Kitabu cha rekodi za Guiness kilituma risala za rambi rambi kwa bawana
Magar kikisema kwamba hakuwacha udogo wake kumzuia kupata maisha bora
duniani.
Bwana Magar alitambulika kuwa mtu mfupi zaidi duniani wakati wa sherehe za kuadhimisha mwaka wake wa 18 wa kuzaliwa mwaka 2010.
Katika sherehe iliowaleta pamoja maafisa wakuu kutoka maeneo tofauti alisema:. Sijichukulii kuwa mtu mdogo.
”Mimi ni mtu mkubwa , natumai kwamba taji hili litanifanya kuthibitisha
hilo ili niweze kupata nyumba nzuri na familia yangu” , alisema wakati
huo.
Kitabu cha rekodi za dunia cha Guiness kina orodha mbili za watu wafupi – wanaotembea na wasio tembea.
Raia wa Ufilipino Junrey Balawing ambaye hawezi kutembea ama hata
kusimama bila usaidizi ndio mtu mfupi zaidi duniani asiyeweza kutembea.
Akiwa na urefu wa sentimita 59.93.
Bwana Magar alipoteza taji lake akiwa mtu mfupi zaidi duniani kwa raia
wa Nepal Chandra Bahadur Dangi ambaye alikuwa na urefu wa sentimita
54.6.
Hatahivyo, alihifadhi taji lake kufuatia kifo cha bwana Dangi 2015.
Bwana Magara kwa mara ya kwanza alionekana na muuzaji mmoja wakati
alipokuwa na umri wa miaka 14 na kuchukuliwa katika maonyesho ya eneo
hilo ambapo watoto walilazimika kulipa fedha ili kupigwa picha naye.
Baada ya kutambulika na kitabu cha rekodi za dunia cha Guiness 2010,
alisafiri maeneo mbalimbali duniani na kuonyeshwa katika vipindi vya
runinga Ulaya na Marekani . Pia ndiye aliyekuwa sura rasmi ya kampeni za
italii huko Nepal .
Craig Glenday, Muhariri wa kitabu cha rekodi za Guiness alisema kwamba
alijawa na majonzi aliposikia habari za kifo cha bwana Magar.
”Alikuwa na tabasamu nzuri ambayo ilimvutia kila mtu aliyekutana naye”, alisema.
Rekodi ya mtu mfupi zaidi duniani anayetembea hivi sasa inashikiliwa na
Edward Hernandez wa Colombia ambaye ana urefu wa sentimita 70.21.
Chanzo – BBC