Mwanahabari aibuka mfanyakazi bora jiji la arusha, apc wampongeza

Wakili Mary Mwita ambaye pia Mwandishi wa habari mkongwe nchini na mwanachama wa Chama cha Waandishi wa Habari Arusha akipokea zawadi ya mfanyakazi bora wa Jiji kutoka kwa Mkuu wa Mkoa wa Arusha John Mongela katika maadhimisho ya siku ya wafanyakazi Mei mosi mwaka huu yaliyofanyika katika viwanja vya General tyre Njiro Arusha
Wakili Mary Mwita pamoja na Mkurugenzi bwa Jiji la Arusha Dkt John Pima wakiwa wameshikilia kikombe cha ushindi 

 Na Seif Mangwangi, Arusha

Chama cha waandishi wa habari Mkoa wa Arusha (APC), kimempongeza mwanachama wake Wakili Mary Mwita kwa kufanikiwa kuchaguliwa kuwa mfanyakazi bora wa Jiji la Arusha.

Akitoa salamu hizo, Mwenyekiti wa APC Claud Gwandu amesema Mary Mwita anastahili nafasi hiyo kwa kuwa amekuwa msaada mkubwa katika jiji la Arusha akisaidia kukusanya mapato ya Serikali.

Amesema Jiji la Arusha limekuwa miongoni mwa majiji yanayofanya vizuri katika idara ya ukusanyaji mapato tangu Wakili Mary Mwita alivyoajiriwa katika Jiji hilo hivyo anastahili pongezi.

“Kwa kweli kazi anayoifanya Mary mwita ni kazi ya kizalendo sana, anakusanya fedha ambazo ndio hizi zinatumika kujenga hospitali, kukopesha wajasiriamali, kukarabati na kujenga shule n.k sisi tunamuomba aendelee kufanya vizuri na Mungu atalipa,”amesema Gwandu.

Gwandu amesema APC inajivunia kuwa na mwanachama huyo kwa kuwa mbali ya kuipatia sifa Jiji la Arusha lakini pia amekuwa akiipatia sifa tasnia ya habari hususani chama cha waandishi wa habari Mkoa wa Arusha.

Amesema Mary Mwita kabla ya kuingia Jiji la Arusha alikuwa kiongozi mwadilifu ndani ya chama cha Waandishi wa Habari Mkoa wa Arusha  akihudumu kama mwekahazina na baadae Mwenyekiti wa Kurugenzi ya nidhamu na maadili na kote alifanya vizuri.

Ametoa wito kwa waandishi wengine wa habari kuiga mwenendo wa Mwandishi Wakili Mary Mwita kwa kujiendeleza kielimu lakini pia kufanya kazi kwa bidii kwaajili ya kuleta maendeleo ya Taifa.