Rc mongela awataka wastaafu mfuko wa psssf kuacha mihemko kuanzisha miradi mikubwa itakayowapa mawazo

Mkuu wa Mkoa wa Arusha, John Mongela akitoa hotuba ya ufunguzi wa semina ya maandalizi ya wastaafu kwa wastaafu watarajiwa wa mfuko wa PSSSF
Kaimu Mkurugenzi wa mfuko wa pensheni wa PSSSF Mbaruku Magawa akimkabidhi Mkuu wa Mkoa wa Arusha John Mongela zawadi wa mti ikiwa ni moja ya kampeni za mfuko huo kupanda miti milioni Moja (1000,000) kufikia Disemba mwaka huu 2023 
washiriki wa semina wastaafu watarajiwa wakifuatilia mada zilizokuwa zikiwasilishwa 
Mkuu wa Mkoa wa Arusha John Mongela akipatia mmoja wa wastaafu watarajiwa zawadi ya mti
Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa PSSSF Mbaruku Magawa akimkaribisha Mkuu wa Mkoa wa Arusha John Mongela
Wastaafu wakifuatilia hotuba ya mgeni rasmi Mkuu wa Mkoa wa Arusha John Mongela(hayupo pichani) ambaye amewataka kujitayarisha mapema kabla ya kustaafu

 

Na Seif Mangwangi, Arusha

SERIKALI imewataka wastaafu wanaotarajia
kustaafu utumishi wao kuanza kufanya maandalizi ya kustaafu kwao mapema ikiwemo
kubuni miradi ambayo wataweza kuifanya baada ya kutoka kazini ili kuwa rahisi
kuiendeleza.

Aidha watumishi hao wametakiwa kutumia
sehemu ya fedha za mafao watakazolipwa baada ya kustaafu kuziwekeza kwenye
miradi itakayowaletea tija na ambayo itaweza kudumu kwa kipindi kirefu na kuepuka kuanzisha miradi kwa mihemko.

Wito huo umetolewa leo Septemba 19,
2023 na Mkuu wa Mkoa wa Arusha, John Mongela alipokuwa akifungua semina ya
maandalizi ya kustaafu kwa wastaafu watarajiwa wa mfuko wa hifadhi ya Jamii PSSSF
wa Mkoa wa Arusha.

Mongela amesema wastaafu wengi
wamekuwa wakipoteza maisha mara tu baada ya kuhitimisha utumishi wao kazini
kutokana na kukutwa na msongo wa mawazo yanayosababishwa na kutojipanga mapema
kabla ya kustaafu.

“Kustaafu utumishi wa umma ni jambo
la lazima sio hiyari lakini lazima ujiulize kabla ya kustaafu umejipanga kuishi
maisha gani baada ya kustaafu?, hili swali ni muhimu sana kujiuliza ili uweze
kuishi maisha marefu zaidi mpaka Mungu atakapokuita,”amesema.

Amesema Serikali inawapenda
wastaafu na ingependa kuendelea kuwatumia mara baada ya kustaafu utumishi wao
hususani kwenye shughuli za kijamii ambazo zinahitaji watumishi wenye maarifa
mengi ambayo wastaafu tayari wanayo.

“Afya zenu ni muhimu sana, kwetu
sisi kama Serikali, tunawapenda na tungependa kuendelea kufanyakazi na nyie,
mkistaafu mtakuwa kijijini ambapo kuna nafasi nyingi za siasa ambazo pia
zinahitaji watu wenye maarifa na uzoefu, tungependa kuona mnaendelea kuwa na
afya nzuri ili muweze kuisaidia Jamii kwenye nafasi kama hizi,”amesema na
kuongeza:

“Ningewashauri mkistaafu msiende
kuanzisha miradi kwa mihemko, miradi mingine ni kukukimbizia kaburini, mfano
umepokea mafao yako unaenda kununua daladala, huu ni mradi ambao unahitaji
kuendeshwa na wazoefu, anzisheni miradi ambayo mtaweza kuifuatilia na hata
kuiendesha wenyewe,”amesema.

Amesema katika semina hiyo taasisi
mbalimbali zimeweza kutoa elimu ya uwekezaji wa fedha ikiwemo taasisi za
kibenki, hivyo ni wakati wao kutafakari kwa makini ni wapi wawekeze kwa faida
kubwa.

Awali akimkaribisha Mkuu wa Mkoa,
Kaimu Mkurugenzi  Mkuu wa mfuko wa PSSSF,
Mbaruku Magawa amesema mfuko wa PSSSF umeamua kutoa elimu ya uwekezaji kwa
wastaafu watarajiwa wa mfuko huo ili kuwajenga kisaikolojia na kuwaondoa kwenye
msongo wa mawazo baada ya kustaafu.

Amesema mfuko huo umeamua kuendesha
semina hiyo baada ya kuwepo kwa matukio mbalimbali ya wastaafu kupoteza maisha
mapema mara baada ya kuhitimisha utumishi wao kutokana na kukosa elimu ya
uwekezaji.

Aidha Magawa amesema mfuko huo unaendesha kampeni ya kupanda miti kote nchini ambapo hadi kufikia Disemba mwaka huu wanatarajia kupanda miti Milioni 1 hadi kufikia Disemba 2027 miti Milioni 7 itakuwa imeshapandwa