Ubunifu wa taasisi ya teknolojia dar es salaam (dit) wamkosha waziri mkuu

 Na Mwandishi Wetu.

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,  Mhe. Kassim Majaliwa amempongeza  mhitimu wa DIT Shahada ya Umeme,  Erasto Chiswanu aliyebuni na kutengeneza kiti cha walemavu ambacho hakihitaji kusukumwa.

Waziri Mkuu alitoa pongezi hizo leo alipotembelea kwenye maonesho ya kilele ya Mashindano ya Kitaifa ya Sayansi, Teknolojia na Ubunifu (MAKISATU) 2021 jijini Dodoma katika uwanja wa Jamhuri.

Aidha, Waziri Mkuu amempongeza pia mbunifu mwingine Adamu Kinyekile ambaye amebuni mashine ya kumsaidia mkulima kuvuta maji, kupukuchua nafaka, kukoboa na kusaga ambayo inatembea na  inamfata mkulima popote alipo.

Mashine hiyo Adamu Kinyekile ametengeneza chini ya usimamizi wa DIT akiwa ni mshindi wa MAKISATU 2019.

Katika hotuba ya Waziri Mkuu ya kufunga maonesho hayo, alisema “nimeona kijana ametengeneza kiti cha walemavu, kumbe tunaweza kutengeneza kiti cha umeme badala ya cha kuchanganya kwa mikono na hii imefanywa na kijana wa DIT, tumpigie makofi”.