Waandishi waombwa kuelimisha jamii umuhimu wa chanjo ya uviko-19

 

Na Mwandishi wetu, Arusha.

Waandishi wa habari nchini ,wametakiwa kusaidia kueleza umuhimu wa Chanjo ya Uviko-19 Kwa watanzania ili wananchi wengi waendelee kuchukuwa tahadhari.

Mwandishi wa habari Mwandamizi, Sammy Awami akitoa mada katika mafunzo ya waandishi wa habari kutoka jamii za pembezoni yaliyoandaliwa na chama cha waandishi wa pembezoni (MAIPAC) kwa ufadhili wa shirika la kimataifa la journalist for human Rights (JHR) alisema bado jamii hasa ya pembezoni Haina elimu ya kutosha ya Uviko-19 na chanjo.

Awami alisema kumekuwepo na habari za upotoshwaji nyingi dhidi ya  Chanjo za Ugonjwa wa Uviko-19 ambazo wanahabari wanapaswa kuelimisha jamii kuwa Dunia ya Sasa haiwezekani kuwa na chanjo inayoweza kuuawa watu ama kuwafanya mazombi.

” Kuna vyanzo vingi vya habari za Uviko-19 kutoka Kwa wataalam wa afya na serikali wanahabari mnapaswa kuvitumia kuepusha huu upotoshwaji” alisema.

Afisa miradi ukanda wa Afrika Mashariki na Kati wa JHR,Siyabulela Mandela alisema wanahabari wanafursa kubwa kuelimisha jamii dhidi ya Uviko-19 na chanjo.

Alisema JHR itaendelea kusaidia wanahabari nchini kuandika habari nyingi za Uviko-19 ili kusaidia jamii kukabiliana na Ugonjwa huo na Taasisi Hiyo itaendelea kusaidia wanahabari kuandika vizuri juu ya Uviko-19.

Mkurugenzi wa MAIPAC Mussa Juma alisema shirika lao limejipanga kushirikiana na serikali na wadau kutoa elimu dhidi ya Uviko-19 na chanjo zake ili kukabiliana na upotoshwaji . 

Juma alisema  katika jamii za pembezoni za Wahadzabe, Masai, Wabarbeig na wengine bado hakuna elimu ya kutosha dhidi ya Uviko-19.

“Katika program hii tumewaita wanahabari kutoka jamii za pembezoni kupata elimu ya Uviko-19 ya masuala ya  haki za binaadamu na usalama wao ili wawe mabalozi Katika jamii walipotoka”alisema

Alisema pia Taasisi hiyo inajipanga kuwakutanisha wanahabari wengine na wataalam Uviko-19 ili kusaidia kuondoa upotoshaji dhidi ya Uviko-19 na chanjo”alisema

Mkufunzi Gasirigwa Sengiyumva alisema Chanjo za uviko-19 zimethibitishwa na shirika la afya Duniani(WHO) na mashirika mengine ya utafiti Hivyo hakuna sababu za kutilia shaka.

“Lakini pia wanahabari lazima tuendelee kuchukuwa tahadhari dhidi ya Uviko-19 ikiwepo kuchanjwa na kutumia vizuizi ili kujikinga na Uviko-19″alisema

Wanahabari kutoka mikoa ya Arusha, Kilimanjaro na Manyara walishiriki mafunzo hayo ya siku tatu jijini Arusha.