Wahukumiwa kunyongwa kwa mauaji ya eva

Na Joctan Mnyeti, Njombe

Mahakama kuu kanda ya Iringa iliyokaa kupitia kikao chake katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Njombe,imewahukumu washtakiwa wawili Mwapulise Mfikwa (29) na Manase Mhada (25) kunyongwa hadi kufa kutokana na kukutwa na hatia ya kumuua Eva Merikion Mgaya (28) nyumbani kwake katika kijiji cha Ihanga wilayani Njombe katika tukio lililotokea Mei8,2015.

 
Katika shauri la Jinai namba 2/2018 la mauaji ya  Eva Merikion Mgaya washtakiwa hao akiwemo Mwapulise Mfikwa mbena ambaye ni mkazi wa Kibaigwa,Dodoma na Manase Mhada mbena mkazi wa Kifanya mjini Njombe,walitekeleza mauaji hayo baada ya kuvamia nyumbani kwa marehemu walipofika kwa lengo la kuiba.
 
Akisoma hukumu hiyo Jaji Filmin Matogolo amesema tukio la mauaji lilitokea huko katika kijiji cha Ihanga mnamo tarehe 8/5/2015 baada ya washatakiwa kwenda nyumbani kwa Wilfred Vitus Ng’olo ambaye ni mume wa marehemu wakiwa na siraha aina ya bunduki shotgun iliyotengenezwa kwa njia za kienyeji inayotumia risasi aina ya 12 bore ambapo walivamia,kuiba na kunyang’anya fedha nyumbani kwa marehemu.
 
Mahakama imeeleza kuwa vile vile washatakiwa walifanikiwa kuchukua simu ya mume wa marehemu na kumpiga risasi Eva Merikion Mgaya kifuani kwa kutumia bunduki hiyo na kusababisha kifo chake papo hapo na kisha kutoweka mpaka walipokuja kukamatwa baada ya upelelezi juu ya mauaji hayo.
 
Jaji Filmin Matogolo amesema washtakiwa hao walitenda kosa kinyume na kifungu cha 196 na 197 cha Kanuni ya adhabu Sura ya 16 Marejeo ya 2019. 
 
Kwa upande wao mawakili wa utetezi Jerome Njiwa na Octavian Mbungali,mara baada ya hukumu hiyo wameiomba mahakama kukabidhi siraha iliyotumika kwenye mauaji kwa jeshi la polisi na simu kurudishwa kwa mume wa marehemu.
 
Pia shauri hilo limeendeshwa na mawakili wa serikali Adrew Mandwa pamoja Matiku Nyangero.