Wananchi waomba chf kuondoa changamoto ya kukosa dawa

 Na Mapuli Misalaba, Shinyanga

Baadhi ya wananchi wa Manispaa ya Shinyanga wamesema upatikanaji wa huduma za matibabu kwenye Bima ya Afya iliyoboreshwa (iCHF) bado kunachangamoto za kukosa dawa ambapo wameiomba serikali kuondoa changamoto hiyo katika  vituo vya Afya 

Wakizungumza kwa nyakati tofauti tofauti wananchi hao wamesema ukosefu wa dawa katika vituo vya afya imekuwa ni changamoto kubwa kwao ambayo inasababisha kutoiamini Bima ya Afya iliyoboreshwa  

Aidha baadhi ya wananchi wamedai kutofikiwa na elimu ya Bima ya Afya iliyoboreshwa (iCHF) ambapo wameiomba  Serikali kuwa  pamoja na maboresho yanayoendelea kwenye Bima hiyo lakini inapaswa kutoa elimu sahihi kwa jamii itakayowahamasisha watu wengi kujiunga na mpango huo 

Mratibu wa Bima ya afya iliyoboreshwa (iCHF) iliyoboreshwa Manispaa ya Shinyanga Bwana Jackson Njau  amesema Halmashauri hiyo imeendelea kuchukua hatua madhubuti na kuongeza kasi ya kuondoa changamoto na kero zinazojitokeza  kwa Wanachama wake katika upatikanaji wa huduma za matibabu

Amesema  halmashauri hiyo imekuwa na jitihada za maksudi  kuhakikisha wanachama wa Bima ya afya iliyoboreshwa  (iCHF)iliyoboreshwa wananufaika na mpango huo kwa kupata huduma bora na stahiki,ili kuondoa malalamiko yanaweza kuzuilika.

“Maboresho sasa hivi ni makubwa tofauti na hapo awali kwa sababu tulikuwa na changamoto kubwa ya upatikanaji wa huduma kwenye vituo vya afya, dhahanati, hosptali za wilaya Kolandoto pamoja na hosptali ya rufaa ya mkoa wananchama wetu walikuwa hawapatiwi huduma stahiki lakini tulivyokuwa tunaendelea katika ufuatiliaji wa kila siku imesaidia sana kukaa na viongozi wa vituo kuweka mikakati kama Halmashauri lakini sasa wameelewa kwahiyo changamoto ya dawa na huduma zile za CHF kwa sasa zimepungua”amesema Njau

Hata hivyo amesema pamoja na jitihada mbalimbali zinazofanyika lakini  bado kuna changamoto inayojitokeza  katika hospitali ya rufaa ya Mkoa wa Shinyanga hasa kwa wanachama waliopata rufaa kutoka vituo vya afya, hali inayochangia baadhi yao kutohuhisha uanachama wao.

“Changamoto kubwa iliyobaki ni upatikanaji wa huduma katika Hosptali yetu ya rufaa ya mkoa kwa sababu wanachama wamekuwa wakienda pale wanaambiwa walipe pesa wengine wanaambiwa kadi hazifanyikazi wengine huduma haipo hii inapelekea yule aliyejiunga kutoona umuhimu tena wa kuhuhisha hizi bima lakini tumejaribu kukaa nao siwezi kusema vibaya huduma zimerejea na wanachama wanaendelea kupata huduma kama kawaida”amesema mratibu Njau

Hivi karibuni Mratibu wa Bima ya Afya iliyoboreshwa (iCHF) Mkoa wa Shinyanga Lyidia kwesigabo alisema uelewa mdogo kuhusu umuhimu wa Bima ya Afya iliyoboreshwa iCHF ni moja ya sababu inayochangia wananchi kutojiunga na mpango huo.