Bodi ambazo hazitawasilisha gawio ifikapo januari 23 zitakuwa zimevunjwa

 Waziri wa Fedha na Mipango, Mhe. Dkt. Philip Isdor
Mpango (Mb), akipokea hundi ya kiasi cha Sh. Milioni 200, kutoka kwa Mkurugenzi
Mkuu wa Taasisi ya Kuthibiti Ubora wa Mbegu Tanzania (TOSCI), Bw. Patrick
Ngwediagi, katikati ni Msajili wa Hazina, Bw. Athumani Mbuttuka, wakati wa
halfa ya kupokea gawio jijini Dodoma.

 Waziri wa Fedha na Mipango Mhe. Dkt. Philip Isdor
Mpango (Mb), akizungumza na vyombo vya habari jijini Dodoma wakati wa hafla ya kupokea gawio la kiasi cha sh. Bilioni 12.12,
kutoka kwa Taasisi 58
zilizotoa gawio kwa Serikali baada ya agizo la Mhe.
Rais Dkt. John Pombe Magufuli, alilolitoa  Novemba 24, Ikulu jijini Dodoma.

 Msajili wa Hazina, Bw. Athumani Mbuttuka, akitoa
taarifa ya kiasi cha fedha ambazo zimepokelewa kutoka kwa Taasisi za Serikali
ikiwa ni kuitikia agizo lililotolewa na Raisi wa Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli kwa Taasisi ambazo hazikuwasilisha gawio
la Serikali Chamwino Ikulu jijini Dodoma.

 Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Wizara ya
Fedha na Mipango, Bw. Benny Mwaipaja, akisoma orodha ya Taasisi za Serikali
ambazo zimetoa  gawio la Serikali
kwa  Waziri wa Fedha na Mipango, Mhe.
Dkt. Philip Isdor Mpango (hayupo pichani), jijini Dodoma.

 Sehemu ya Wawakilishi wa Taasisi waliofika kwa ajili
ya kutoa gawio la Serikali wakisikiliza hotuba ya Waziri wa Fedha na Mipango
Mhe. Dkt. Philip Isdor Mpango (Mb), (hayupo pichani), wakati wa hafla ya
kupokea gawio jijini Dodoma.

Waziri wa Fedha na Mipango Mhe. Dkt. Philip Isdor
Mpango (Mb), (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Wenyeviti mbalimbali na
Watendaji Wakuu kutoka Taasisi za Serikali baada ya halfa ya kukabidhi gawio la
kiasi cha Sh. Bilioni 12.12 kutoka kwa Taasisi 58 jijini Dodoma. kutoka kushoto
ni Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Mipango Bw. Adolf Ndunguru, kwa
niaba ya Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, 
kulia ni Msajili wa Hazina, Bw. Athumani Mbutuka

(Picha na Josephine Majura – WFM Dodoma).

Na Peter Haule na
Josephine Majura, WFM, Dodoma
Serikali imesema  Bodi na Watendaji Wakuu wa Mashirika, Kampuni
na Taasisi za Umma ambazo hazitawasilisha gawio na michango yao kwenye Mfuko
Mkuu wa Serikali  ifikapo Januari 23
mwaka 2020, kabla ya saa 6 usiku, Bodi zitakuwa zimevunjwa na watendaji wake
kupoteza ajira zao.
Hayo yameelezwa Jijini
Dodoma na Waziri wa Fedha na Mipango Dkt. Philip Isdor Mpango, wakati akipokea
gawio na michango kutoka Mashirika, Kampuni na Taasisi za Umma 11, ikiwa ni
utekelezaji wa agizo la Mhe. Rais Dkt. John Pombe Joseph Magufuli alilolitoa
Novemba 24 mwaka huu lililozitaka taasisi hizo kutoa gawio ndani ya siku 60.
Alisema itakapofika saa
sita usiku ya tarehe 23 Januari, 2020 kama hawajaleta gawio wala michango ya
kuingia kwenye mfuko Mkuu, Bodi hizo zimevunjwa, Watendaji Wakuu wa hizo
taasisi husika nao watahusika na akabainisha kuwa hiyo ndiyo amri ya Serikali.
 “Tukio la Novemba 24, 2019 la kupokea gawio,
mashirika yalikuwa 79 na Mhe. Rais, alipokea hundi ya jumla ya Sh. trillion
1.05 na aliniagiza ndani ya siku 60, Taasisi, maashirika na kampuni 187 ambazo
hazikutoa gawio siku hiyo zitekeleze maagizo yake”, alieleza Dkt. Mpango.
Alisema kuwa baada ya
agizo la Rais, katika kipindi cha siku 18, Taasisi, Kampuni na Mashirika 58
yametekeleza agizo ambapo jumla ya fedha zilizopokelewa katika mfuko Mkuu wa
Hazina ni Sh. bilioni 12.12.
Dkt. Mpango aliyapongeza
mashirika, kampuni na taasisi hizo kwa kuitikia wito huo kwa kutoa fedha hizo
ambazo amesema zitasaidia katika shughuli za maendeleo  ya nchi kwa njia ya ujenzi wa miradi na
kuiwezesha nchi kujitegemea.
Alisema kuwa amefurahishwa
na gawio na michango lakini amesema wanatakiwa kuongeza kiwango hicho mwakani
kwa kuwa Watanzania wanatakiwa kuona kuwa waliopewa  dhamana 
ya kusimamia mashirika yao wanatimiza wajibu wao.
Kwa upande wake Msajili wa
Hazina Bw. Athumani Mbutuka, amesema idadi ndogo ya kampuni, mashirika na
taasisi ya umma 71 kati ya 266 yaliyo katika orodha ya Msajili wa Hazina
yaliyochangia gawio na michango mingine wakati Mhe. Rais Magufuli akipokea
magawio hayo kwa niaba ya  wananchi,
haikumfurahisha Kiongozi huyo wa Nchi.
Miongoni mwa Taasisi
zilizotoa mchango ni pamoja na Chuo cha kilimo- SUA, Chuo cha Mipango na
Maendeleo Vijijini- IRDB, Taasisi ya Taifa ya 
Usafirishaji – NIT, Mfuko wa Misitu Tanzania- TFS, Chuo cha Ufundi
Stadi- VETA, Mamlaka ya Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali na Taasisi ya Kudhibiti
ubora wa Mbegu Tanzania.