Diwani agawa barakoa, vitakasa mikono

Diwani
wa kata ya Bomambuzi na Mjumbe wa Kamati ya Fedha na Uongozi  Manispaa
Ya Moshi Juma Raibu akiwafundisha wananchi namna ya kuvaa
barakoa(picha na Woinde Shizza, Kilimanjaro)
Na Woinde Shizza , KILIMANJARO

Diwani
wa kata ya Bomambuzi na Mjumbe wa Kamati ya Fedha na Uongozi  Manispaa
Ya Moshi Juma Raibu amekabidhi Barakoa 100, vitakasa Mikono,  pamoja na
Ndoo Kwa wafanyabiashara wa Soko la pasua Mjini Moshi ili kujikinga na maambukizi ya Virusi vya
Corona  ambavyo vinaendelea kutikisa dunia.

Akiongea
wakati  akikabidhi vifaa hivyo Diwani huyo alibainisha kuwa ameamua
kutoa vifaa vya kujikinga na ugonjwa wa Corona kwa wananchi hao ,ili waweze kuokoa maisha yao na kuwa na tahadhari ya ugonjwa huo wakati wote.

Amesema
kuwa mbali na kutoa vifaa hivyo pia ameweza kugawa elimu ya kujikinga
na ugonjwa hatari wa Corona kwa wananchi wa kata ya Bomambuzi pamoja
na wafanyabiashara wa masoko ya pasua na  mbuyuni huku akibainisha
kuwa wataendelea kutoa vifaa vya kujikinga na elimu kwa kila mwananchi.

Aidha
aliwaasa Wananchi hao kufuata Maelekezo ya Wataalamu wa Afya na Maagizo
Ya Serikali huku wakizingatia zaidi  Kuepuka Misongamano Isiyo Ya
Lazima. 

Pia
Diwani huyo aliwaonya wananchi wanaopotosha jamii kuhusu  idadi ya
wagonjwa pamoja na  wanaofariki kwa virusi vya Corona na kusema kuwa 
iwapo atabainika mtu anafanya hivyo hatua Kali zitachukuliwa dhidi yake,
huku akiliagiza jeshi polisi kuwachukulia hatua kali za kisheria.



Amesema
wamehamasisha jamii juu ya kuweka na kunawa na maji tiririka na sabuni
kwenye sehemu zote za biashara nyumbani na maeneo yote yenye
mikusanyiko.


Akishukuru
kwa msaada huo mmoja wa  wafanyabiashara wa soko la Pasua Gloria Mboya
alisema kuwa anashukuru kwa diwani huyo kwa kuendelea kuwajali wananchi
wake  kwa kuwapa vifaa vya kujikinga pamoja na kuwapa elimu ya namna ya
kuendelea kuchukuwa tahathari ya ugonjwa huo.

Alisema
kuwa ugonjwa huo upo hivyo ni vyema kila mtanzania  kuendelea kujikinga
na kufuata maelezo yanayotolewa na wataalam,huku akikisitiza kuwa iwapo
mtu yeyote akijihisi anadalili za ugonjwa huo kuwa maramoja hospital
kwa ajili ya kupata  huduma.