Mbunge neema lugangira afanikisha msaada wa vipima oxygen vituo vya afya mikoa 11

 


RAIS wa DICOTA Dkt Frank Minja,Naibu Waziri wa TAMISEMI anayeshughulikia Masuala ya Afya; Mhe Dkt Festo Dugange,Naibu Katibu Mkuu Afya na Mbunge wa Viti Maalumu (CCM) Kundi la Asasi za Kiraia (NGOs) Mh Neema Lugangira wakifungua vipimo vya Oxijeni ili kujaribu ufanyaji kazi wake

Baada ya kukabidhiwa wanaviangalia vipima Oxijeni hivyo

MBUNGE wa Viti Maalumu (CCM) Kundi la
Asasi za Kiraia (NGOs) Mh Neema Lugangira na Rais wa Baraza la
Watanzania wanaoishi Marekani (DICOTA) leo wamekabidhi msaada wa Vipima
Oxijeni (Pluse Oximeters) 108 kwa Ofisi ya Rais TAMISEMI kwa ajili ya
Vituo vya Afya kutoka Mikoa 11 ikiwa ni mchango wao katika kuthamini
juhudi za Serikali katika kuimarisha Afya za Watanzania.

Msaada
huo umepokelewa na Naibu Waziri wa Ofisi ya Rais TAMISEMI
anayeshughulikia Masuala ya Afya; Mhe Dkt Festo Dugange  ambapo vifaa
hivyo vitagawiwa katika mikoa ya Dar-es Salaam, Dodoma, Kigoma, Kagera,
Kilimanjaro, Arusha, Tanga, Ruvuma, Mbeya, Lindi na Njombe.

Akizungumza
baada ya kukabidhi msaada huo wa vifaa, Mbunge wa NGOs Tanzania Bara,
Mhe Neema Lugangira alimshukuru Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais TAMISEMI,
Mhe Ummy Mwalimu kwa ushirikiano mkubwa aliowapatia katika kufanikisha
shughuli hiyo ya leo.

Mbunge
Neema Lugangira alisema pia wanashukuru Dkt Grace Maghembe, Naibu
Katibu Mkuu na Dkt Ntuli Kapologwe, Mkurugenzi wa Idara ya Masuala ya
Afya, Lishe kwa ushirikiano wao mkubwa ambao wamekuwa wakiendelea
kuwapatia.

“Sisi
tunamshukuru sana Waziri wa Nchi OR TAMISEMI Mhe. Ummy Mwalimu, kuridhia
kupokelewa kwa msaada huu, ambao umepokelewa na Naibu Waziri, Dkt.
Festo Dugange. Mimi kama Mbunge nitaendeleza jitihada hizi kwa niaba ya
Serikali ili lengo la kuimarisha Afya ya Mtanzania iweze kutimia,”
Alisema Lugangira.

Awali
akizungumza wakati akiipokea msaada huo wa vifaa tiba ambavyo vinatumika
kupima kiasi cha Oxijeni katika mwili wa mwanadamu, Naibu Waziri Ofisi
ya Rais TAMISEMI anayeshughulikia afya, Mhe Dkt. Festo Dugange
amewapongeza Watanzania hao waishio Marekani kwa kuthamini juhudi za
Serikali ya Nchi yao za kujenga na kukarabati miundombinu mbalimbali ya
afya nchini.

Alisema ili
kuhakikisha kuwa jukumu hilo linatekelezwa kikamilifu, Naibu Waziri
ameongeza kuwa katika bajeti ya mwaka 2021/22 serikali imetenga shilingi
bilioni 65 kwa ajili ya kununulia dawa na vifaa tiba.

“Serikali
imefanya kazi kubwa ya ujenzi wa Miundombinu na katika mwaka wa fedha
2021/22 tumeweka kwenye bajeti ya dawa na vifaa tiba kama hivi na
vingine kiasi kinachofikia Bil.65, hivyo kwa jitihada hizi za wadau hawa
na wengine wote watakao kuja hapo baadaye ni ishara kwamba lengo letu
la kuweka vitendanishi na dawa litatimia,” amesema Mhe Naibu Waziri Dkt.
Dugange.

Akiongea kwa
niaba ya Watanzania waishio nchini Marekani, rais wa DICOTA, Dkt. Frank
Minja, amesema, wanaona fahari ya kuchangia vifaa hivyo ambavyo
vitakwenda kugawiwa kwenye ngazi ya Hospitali za Wilaya na kutumika na
watanzania wenzao na kuahidi ni mwanzo ambapo wanatarajia kufanya mengi
zaidi kwa kushirikiana na Serikali na Mbunge Lugangira katika Sekta hii
ya Afya.

Naye Naibu
Katibu Mkuu Ofisi ya Rais TAMISEMI anayeshughulikia Afya Dkt. Grace
Magembe, amesema kuwa atahakikisha kuwa vifaa vilivyopokelewa vinatunzwa
ili viweze kudumu kwa muda mrefu.

Hafla
ya kukabidhi vifaa tiba ilifanyika Makao Makuu ya Ofisi ya Rais
TAMISEMI jijini Dodoma na kuhudhuriwa pia na Mkurugenzi wa Huduma za
Afya, Lishe na Ustawi wa Jamii kutoka Ofisi ya Rais TAMISEMI Dkt. Ntuli
Kapologwe na Katibu Mtendaji wa Tume ya Utumishi wa Walimu Paulina
Mkwama.