Mwimbaji wa injili amuua mkewe kwa kumkata shoka

Jeshi la Polisi Mkoa wa Arusha nchini
Tanzania linamtafuta Moses Pallangyo akidaiwa kumuua kwa kumkata shoka
mkewe Marry Richard Mushi mkazi wa kijiji cha Kilinga wilayani Arumeru
mkoani humo.

Kamanda wa polisi mkoa Arusha, Jonathan Shana amesema tukio hilo
limetokea leo Jumatano Desemba 25, 2019 mchana kutokana na ugomvi wa
kifamilia.
“Baada ya kufanya mauaji ametoroka na tunamsaka lakini chanzo kamili cha
ugomvi hakijulikani lakini taarifa za awali zinaeleza huenda ni wivu
wa mapenzi,” amesema Shana
Pallangyo ambaye ni maarufu kwa jina la Moses Lebaba ni mwimbaji wa kwaya za Kiinjili mkoani Arusha.
Baba wa mtuhumiwa, Latiaeli Pallangyo anasema tukio hili limetoka ikiwa
ni wiki tatu tangu marehemu aanze kuishi na mwanae kama mke na mume.
“Hapakuwapo na ugomvi wowote na walitegemea kusherehekea sikukuu ya
Krisimasi vizuri. Mara baada ya Marry kupika chai aliendelea na
shughuli za kawaida mpaka mauti yalipomfika kwa kupigwa na shoka
chumbani kwake,” amesema