Serikali yatoa kauli mahindi kupanda bei

Serikali imesema licha ya bei ya mahindi kuwa juu, haitaingilia kupunguza bei kwani ni nafasi ya wakulima kupata bei wanayotaka.

Naibu Waziri wa Kilimo nchini Tanzania, Hussein Bashe ametangaza msimamo
huo bungeni leo Jumatatu Novemba 11, 2019 wakati akijibu swali la
nyongeza la Mbunge wa Busega (CCM), Dk Rafael Chegeni.

“Sasa hivi bei ya vyakula inazidi kupanda na ukiangalia wananchi wengi
wanaadhirika na hali hii, gunia la mahindi sasa ni karibu Sh. 100,000 je
serikali ina mkakati gani wa kupunguza gharama hizi kwa wananchi,”
alihoji Dk. Busega.

Akijibu swali hilo Bashe amesema msimamo wa serikali ni kutokuingilia
kushusha bei ya mazao kwa kuwa wakulima wameshapata hasara na hivyo
watapunguza gharama za uzalishaji na kuruhusu ushindani katika soko.

“Hatutaingilia kupunguza bei ya mazao kwasababu wakulima wa nchi hii kwa
muda mrefu wamepata hasara, huu ni msimamo wa serikali na ieleweke
hivyo, njia ya pili tunahamsisha Watanzania kuongeza uzalishajikwani
supply ikiwa kubwa demand ikiwa ndogo mazao yatashuka bei.

“Ni bunge hili hili mwaka jana wakati bei ya mahindi kwa mkulima ilikuwa
sh. 150 wakasema kwanini tunafunga mipaka, sisi kama serikali hatua
tunazozichukua kupunguza gharama za bei sokoni ni pamoja na kupunguza
gharama za uzalishaji, kuruhusu soko kushindana, kwahiyo hatutaingilia
kushusha bei, tunayo National Food Reserve Agency na niwaambie wabunge
na wakuu wa mikoa pale wanapoona kuna upungufu wa mazao ya chakula
sokoni wawasiliane na mawakala hao ili wasambaze chakula katika maeneo
hayo,” amesema Bashe.