Mavunde: wawekezaji wazawa sekta ya madini acheni majungu

Anthony Mavunde, Waziri wa Madinj

Wawekezaji katika sekta ya Madini wametakiwa kuacha majungu na kusemana maneno ya uongo badala yake wawe na umoja na kupeana mbinu za kuinuana kifikra ili wazidi kustawisha uchumi wao na Taifa kwa ujumla.

Akifungua Mkutano wa Jukwaa la Tatu la Utekelezaji wa Ushirikishwaji wa Watanzania katika Sekta ya Madini Jijini Arusha, Waziri wa Madini Anthony Mavunde amesema Serikali ipo tayari kushirikiana na Watanzania wote wenye nia njema ya kukuza sekta ya Madini nchini.

“Eneo jingine ambalo serikali itahakikisha inatoa sapoti ni pamoja na kujenga maabara kubwa ya upimaji madini jijini Dodoma, na kwa mwaka wa fedha utakaoanza Julai Wizara inatarajia kufanya ununuzi wa helikopita itakayofungwa vifaa mahususi vya kutafiti na kugundua madini yalipo na wingi wake,”Amesema.

Aidha Mavunde amesema pamoja na kwamba sekta ya Madini imezidi kukua na kufikia asilimia tisa kwa pato la Taifa, hivyo amewataka Watanzania wote wenye Hati Madini kufuata sheria, kanuni, taratibu na kuacha kutoa mikataba bila kutangaza zabuni.

“Ndugu zangu Wawekezaji wa Sekta ya Madini huu mkate ni mkubwa, huwezi kula peke yako kikubwa timiza majukumu yako kwa sehemu yako, tengenezeni sauti moja ili mratibiwe kwa urahisi, acheni kuvutana bali atakayefanikiwa amsaidie na mwingine, na kipekee naipongeza TAMESA kupitia PSSSF imekuwa mfano bora wa kuigwa”,

“Pia Wizara tunajipanga kuhakikisha manunuzi ya bidhaa za madini yanafanyika hapa nchini kwa kuzungumza na wawekezaji kuwekeza hapa nchini ili bidhaa zote muhimu zinunuliwe hapahapa, pesa ibaki hapa kwetu kukuza uchumi, mfano kila mwaka manunuzi ya bidhaa za madini kwa migodi yote hufikia tilioni 7 za Kitanzania” amefafanua Mavunde.

Wawekezaji Sekta ya Madini wanaojishughulisha na Utengenezaji wa Vifaa Umeme vinavyotumika katika shughuli za Kuchimba Madini (TANALEK)

Katika ufafanuzi huo Mavunde amesema Wizara inaendelea kukamilisha utaratibu wa kufanya maonyesho ya Madini ya Tanzanite na Vito Jijini Arusha kama ilivyokuwa hapo awali ili Watanzania wanufaike.

Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Paul Makonda

Kwa upande wake Mkuu wa mkoa wa Arusha Paul Makonda amewasihi Wawekezaji Sekta ya Madini kuwekeza mkoani Arusha ili kuinua uchumi zaidi kupitia Utalii kwa kutembelea vivutio mbalimbali vilivyopo mkoani humo.

“Nawaombeni Wawekezaji wa Sekta ya Madini msiishie tu kwenye mkutano huu, lakini pia wazeni kuwekeza hapa hasa upande wa kujenga Hoteli, kwani tunatarajia kupata idadi kubwa ya watalii kutoka pande mbalimbali za dunia na vyumba vya kulala wageni havitoshi” ameeleza Makonda.

Wawekezaji wa Sekta ya Madini wakiwa katika Jukwaa la Tatu la la Utekelezaji wa Ushirikishwaji wa Watanzania katika Sekta ya Madini Jijini Arusha

_Hata hivyo Mbunge wa Jimbo la Arusha Mrisho Gambo amezitaka Taasisi mbalimbali za kibenki kuangalia namna ya kupunguza riba kwa wawekezaji wazawa ili wainue uchumi wao na watanzania wengine kuanzia ngazi ya kaya na Taifa kwa ujumla. 

“Wawekezaji wengi wamekuwa wakikwama kuendesha shuguli zao sawasawa kutokana na kuyumba kwa mitaji, lakini Taasisi za kibenki tafakarini hili mkae na wawekezaji hawa ili kuona namna ya kufanya maana uchumi ukikua ni faida yetu sote” amesema Gambo.

Kwa Upande wa Wawekezaji wakiwemo watengenezaji wa vifaa vya umeme vinavyotumika katika shughuli za uchimbaji Madini (TANALEK) wamesema jukumu lao ni pamoja na kutoa mafunzo wa Wachimbaji namna Bora ya kutumia vifaa vya umeme vinavyotengenezwa na TANALEK.

Mhandisi Joseph Tiba kutoka TANALEC ameeleza namna Kampuni hiyo inavyo fanya kazi na Sekta ya Madini Kwa kutoa mafunzo kwa Wachimbaji wamiliki na kutengeneza vifaa vya umeme vinavyotumika katika migodi Mbalimbali nchini.

“Sisi kama TANALEK tunatoa mafunzo kwa wamiliki wa migodi Wachimbaji na tunawaalika kuleta changamoto zitokanazo na uchimbaji Kwa kuwa kazi yetu tunabuni na kutengeneza vifaa kulingana na uhitaji kamili unaopatikana katika migodi” amesema Tiba.

>Jukwaa hilo limebeba Kaulimbiu “Uwekezaji wa Viwanda vya Uzalishaji wa Bidhaa za Midogini kwa Maendeleo Endelevu”.