Viongozi wa klabu za waandishi wa habari wakumbushwa majukumu yao

Na Mwandishi Wetu, Dodoma

Viongozi wa Klabu za Waandishi wa habari nchini, wametakiwa kusimamia dhamana waliyonayo kwa wanachama, kuwa wawazi pamoja na kusimamia utelekezaji wa maazimio yaliyowekwa ili kupunguza migogoro ambayo imekuwa inaibuka mara kwa mara kwenye klabu hizo.

Wito huo umetolewa Leo Jijini Dodoma na Rais wa UTPC Deo Nsokolo, katika hotuba yake ya ufunguzi wa kikao kazi kwa viongozi wa juu wa klabu za Waandishi wa Habari nchini.

Nsokolo amesema haridhishwi na utendaji wa baadhi ya viongozi wa klabu kwa kushindwa kutoa taarifa kwa wakati au kushindwa kutoa mbinu za kutatua migogoro ambayo imekuwa inaendelea kwenye klabu na kupoteza muda mwingi wa kuitatua.

Aidha Rais amesema kuwa, mchakato wa kutafuta raslimali fedha ni mgumu sana kwa sasa na hivyo migogoro hii inaongeza au kuchangia zaidi ugumu wa kutafuta fedha kwa kuwa muda mwingi unatumika kutatua migogoro.

Amewashauri wa viongozi wa klabu kuanza upya kupatana na kufanya kazi pamoja, ili kuongeza tija kwenye kazi yao ya uongozi. 

“Kama kuna kusigana basi uwe nje ya utendaji wa shughuli za klabu kwa kuwa kwa namna moja ama nyingine migogoro ina adhiri utekelezaji wa shughuli za klabu lakini pia inazuia klabu kupiga hatua” Deo Nsokolo

Amesema viongozi wa Klabu za Waandishi wa Habari wanapashwa kuziongoza klabu hizo kwa kufuata miongozo ambayo kila klabu imejiewekea.

 “asitokee kiongozi anaongoza klabu kwa matakwa yake mwenyewe au kwa manufaa yake mwenyewe kwani huyo atakuwa hafai kuwa miongoni mwetu na atakuwa hatutakii mema hasa wakati huu ambao taasisi yetu inafanya mabadiliko makubwa, ni lazima viongozi wa klabu wazingatie utawala bora wakati wote” Deo Nsokolo

Mkutano huo umekutanisha jumla ya viongozi 84 kutoka klabu za waandishi wa habari 28 Tanzania nzima ambao pia wamepata fursa ya kushiriki  kwenye maadhimisho ya Siku ya Uhuru wa Vyombo vya habari Duniani ambayo Kitaifa imefanyika Jijini  Dodoma.