Makamu was rais atangaza kifo cha rais john pombe joseph magufuli

 

Rais Dkt John Pombe Magufuli

Makamu wa Rais Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan ametangaza kifo cha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli kilichotokea leo Jumatano Machi 17, 2021 katika hospitali ya Mzena mkoani Dar es Salaam alipokuwa akipatiwa matibabu.


Rais Dkt. Magufuli amefariki dunia kutokana na maradhi ya moyo ambayo yamekuwa yakimsumbua kwa takribani miaka 10.

Dkt. Magufuli alifikishwa katika Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI) Machi 6 mwaka huu na kuruhusiwa Machi 7, akaendelea na majukumu yake.

Hata hivyo, alipelekwa katika Hospitali ya Mzena Machi 14 baada ya kueleza kujisikia vibaya, ambapo amekuwa akipatiwa matbabu hadi umauti ulipomkuta.

Kufuatia msiba huo, Makamu wa Rais ametangaza siku 14 za maombolezo ambapo bendera zitapepea nusu mlingoti.