Dc mboneko azindua kiwanda cha nyama shinyanga, atoa wito vijana kujitokeza kuomba ajira

 Na Mapuli Misalaba, Shinyanga 

Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga Jasinta Mboneko amezindua rasmi mradi mkubwa wa Machinjio ya kisasa iliyojengwa katika eneo la Ndembezi Manispaa ya Shinyanga,tayari kwa kuanza uzalishaji, baada ujenzi wake kukamilika.

Akizungumza na hadhara ya viongozi,na Wananchi waliohudhuria katika hafla hiyo amesema kukamilika kwa mradi huo mkubwa inatoa fursa mbalimbali kwa Wananchi wa Mkoa wa Shinyanga na maeneneo mengine. 

Mboneko amewaomba wananchi wa mkoa wa Shinyanga kujitokeza  kwa wingi kuomba ajira ambapo amewasisitiza kuchangamkia fursa hiyo, kuwa waaminifu pamoja na kufuata sheria na taratibu zitakazowekwa katika mradi huo ikiwemo kuzingatia muda wa kazi.

“Niwaomba sana wananchi tutumie machinjio hii itakuwa inachinja Ng’ombe na Mbuzi lakini pia niwaombe sana wananchi tujitokeza kuomba nafasi ambazo zitatolewa kwa ajili yenu  niwasihi sana kwanza kwenye kuwahi kazini pili tuzingatie uaminifu na uadilifu kwenye kazi wezi hatutaki we njoo hapa ufanye kazi upate halali yako”

”Wachinjaji wote walioko katika Manispaa yetu ya Shinyanga tuhakikishe tunaitumia machinjio hii hatutaki kuona wananchi wanapata nyama za ajabu ajabu nyama zote zitakazokuwa zinapatikana kwenye bucha zitakuwa zinatokea kwenye machinjio hii  na machinjio hii imezingatia taratibu zote zikiwemo taratibu za afya” 

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Shinyanga Jomaary Satura amesema kuanza kwa uzalishaji wa machinjio ya kisasa, itabadili mfumo wa wafanyabiashara Mkoani Shinyanga ambapo watatakiwa kusafirisha nyama badala ya Ng’ombe kama ilivyozoeleka, ili kwenda sanjari na mahitaji ya soko la sasa.

 Satura amesema ujenzi wa mradi wa Machinjiyo ya kisasa ni sehemu ya mpango wa Serikali ya kuboresha miji na majiji ambao ulianza tangu Mwaka 2012 na umegharimu kiasi cha Shilingi Billioni 5.2 ambapo amesema machinjio hiyo itakizi mahitaji yote ya wananchi wa mkoa wa Shinyanga pamoja na kutoa fursa mbalimbali.

“Pamoja na huduma kwa jamii machinjio hii inaenda kutengeneza ajira kwa vijana wetu wengi tunaweza kuchinja Ng’ombe mia mbili na Mbuzi zaidi ta miatatu kwa siku kwahiyo watu wenye sifa lakini  pia watu wenye elimu zakawaida watapata ajira kwa mtu ambaye ataendelea kuchinja nje ya machinjio hii maana yake ni kwamba amekusudia kuwanyima haki ya msingi wananchi wa Manispaa ya Shinyanga ya kupata nyama ambayo imeandaliwa katika mazingira safi na salama huyo hatuwezi kumkubalia hatu za kisheria zitachukuliwa”.

Akizungumza kwa niaba ya mbunge wa jimbo la Shinyanga mjini Patrobas Katambi muwakilishi wake Samweli Jackson ameiomba ofisi ya mkurugenzi wa Manispaa ya Shinyanga kutoa kipaumbele cha fursa kwa wakazi wa mkoa wa Shinyanga.

“Kwanza niipongeze serikali kwa kuharakisha haya machinjio  yazinduliwa kwa sababu ilikuwa ni kiu kubwa kwa wananchi wa Manispaa Shinyanga kuona fedha zilizowekwa na serikali zinaaza kutumika na wananchi wanufaike ombi langu na rai yangu kwenye ofisi ya Mkurugenzi ni kuona sasa machinjio hii ambayo wananchi wameizunguka wanapatiwa ajira itawanufaisha wao na kuhakikisha wao wanalinda hili eneo”. 

Naye diwani wa kata ya Ndembezi Victor Thobias ameishukuru serikali kwa kushirikiana na uongozi wa Manispaa ya Shinyanga kuelekeza mradi huo katika kata hiyo ambapo ameahidi kuusimamia mradi huo huku akiwaomba wananchi kuonesha ushirikiano wa dhati ili kuleta maendeleo ya mkoa na Taifa kwa ujumla.

Kwa upande wao wananchi waliohudhuria kwenye uzinduzi wa Mradi huo wa machinjio ya kisasa katika kata ya Ndembezi wameiomba Serikali kutoa kipaumbele cha fursa ya ajira kwa Wanachi wazawa.