*dkt. abbasi aongoza mapokezi twiga stars*

Na Mwandishi Wetu

Serikali imewaahidi wachezaji wa Timu ya Taifa ya Wanawake (Twiga Stars), kuwapa zawadi itakayoonesha thamani ya heshima waliyoliletea Taifa baada ya kutwaa ubingwa wa Cosafa nchini Afrika Kusini.

Hayo yamesemwa jana Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Dar es Salaam na Katibu Mkuu wa Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dkt. Hassan Abbasi, aliyeiwakilisha Serikali kuipokea Timu hiyo usiku huu.

“Siku ile tunawaaga mliahidi ubingwa leo mmetimiza ahadi yetu na mmerejea mkiwa mashujaa wa Taifa. Sasa kazi iko kwetu kuwaenzi na Mhe. Rais Mama Samia Suluhu Hassan ameshawapongeza na ameahidi atawaenzi na kutambua mchango wenu sasa tusubiri ahadi yake,” alisema Dkt. Abbasi.

Wakati Serikali na wadau wengine wakiendelea kuipongeza Timu hiyo Dkt. Abbasi amesema kesho wachezaji hao wataandaliwa chakula maalum cha jioni jijini Dar es Salaam ambapo Serikali na wadau watatangaza zawadi mbalimbali zitakazotolewa kwa timu hiyo.