Vijana wapewa wito kujiunga na vikundi vya kikanisa ili kujijenga kiimani

Kiongozi wa Viwawa Shinyanga

 Na Mapuli Misalaba, Shinyanga

Vijana wakatoliki wafanyakazi (VIWAWA) wamewataka vijana wenzao kote nchini kujiunga na na vikundi vya vijana katika kanisa ili kujijenga kiimani na kujiepusha na makundi ya mtaani ambayo yamekuwa na matokeo mabaya.

Wakizungumza kwenye  kongamano la vijana linaloendelea katika ukumbi wa vijana senta Ngokolo mjini Shinyanga, vijana hao wamesema kongamano hilo litawasaidia kukua kiimani pamoja na kujenga familia iliyobora.

Viwawa wakiwa katika kongamano la kuwajenga kiimani

Wamesema kuwa kongamano hilo  limewapa mwanga na uimara wa kuishi katika maisha yanayompendeza mwenyezi Mungu pamoja na kujishughulisha na shughuli mbalimbali kutokana na elimu ya ujasiriamali wanayoipata…

Kwa upande wake mwenyekiti wa VIWAWA jimbo katoliki la shinyanga ambaye pia ni mwenyekiti wa uchumi,mipango na fedha Taifa, Leonard Mapolu ametoa wito kwa vijana wenzake kujiunga na chama hicho cha kitume ili kupata elimu kuhusiana na mambo mbalimbali yanayohusu vijana ikiwemo elimu ya ndoa pamoja na elimu ya kuishi katika maisha ya kikristo.

“Sasa hivi tunaendelea na kongamano la kwanza la VIWAWA jimbo katoliki la Shinyanga ambalo limeanza tangu jana na linaendelea leo na kuhitimishwa Jumapili nitumie fursa hii kuwakaribisha vijana wote wa katoliki kusherehekea sikukuu hiyo ambayo ni sikukuu yao lakini pia tunawakaribisha waumini wengine na watu wote wenye mapenzi mema kujumuika nasi katika sikukuu hiyo kwa kuwa tumelenga kuwapa elimu vijana kuhusu mambo mtambuka  ambayo yanawahusu vijana kwanza yanawajenga hasa kwa pande zote mbili upande wa kiroho na kimwili”

Aidha kongamano hilo la vijana lililoanza siku ya jana litahitimishwa kwa misa takatifu ambayo itaongozwa na mgeni rasmi ambaye ni askofu wa jimbo katoliki la shinyanga mhasham Liberatus Sangu.