Baraza la madiwani chamwino wakataa kupokea taarifa

Na.Mwaandishi Wetu,Chamwino

BARAZA la Madiwani Wilaya ya
Chamwino, Mkoani Dodoma , limekataa kupokea na kujadili taarifa zote za
kamati za kudumu za Halmashauri hiyo na kuagiza kuchukuliwa hatua za
kisheria Mwandishi wa vikao (CC), Bernard Luhamu, wakimtuhumu kughushi
saini za wenyeviti hao wa kamati.

Hii imefatia baada ya wenyeviti
wote wa kamati za kudumu, ikiwemo ile ya Fedha, Uongozi na Mipango
inayoongozwa na Mwenyekiti wa Halmashauri hiyo, Samwel Kaweya,
kushangazwa na hatua ya makablasha hayo kuonekana kusaini kwa saini zao,
wakati hawakuwahi kusaini.

Hatua hiyo ilitokea  juzi katika
kikao cha Baraza la madiwani, kilichoketi kwa ajili ya kupokea na
kujadili taarifa ya utekelezaji za kamati za kudumu kwa kipindi cha robo
ya kwanza kwa mwaka wa fedha 2019/20.

Madiwani hao walimtuhumu mwandishi
huyo wa vikao (CC) kuwa alidiriki kulidanganya Baraza kwa kughushi
saini za Wenyeviti wa kamati hizo za kudumu, huku wakitilia mashaka
baadhi ya vipengele vya taarifa iliyowasilishwa kikaoni hapo
kunyofolewa.

Awali kabla ya Madiwani hao
kufikia uamuzi huo wa kuikataa taarifa hiyo, Diwani wa kata ya Buigiri,
Kenneth Yindi, aliomba muongozo, akihoji kutoonekana kwa baadhi ya
taarifa.

Akijibu hoja ya muongozo huo,
Makamu Mwenyekiti wa Halmashauri hiyo, Elias Kaweya, alikiri kutoonekana
kwa baadhi ya vipengele vilivyojadiliwa kwenye kamati ya fedha.

“Mwenyekiti niwe mkweli juu ya
hili, mimi kama mjumbe wa kamati ya fedha kuna mambo tuliyajadili kule
na yalitakiwa kuwasilishwa kwenye kikao hiki cha baraza lakini
havionekani”.

Kutokana maelezo hayo ndipo
aliposimama Mwenyekiti wa Halmashauri hiyo, Samweli Kaweya na kukiri
kuwepo kwa tatizo hilo la baadhi ya taarifa kunyofolewa, huku
akishangazwa na hatua ya taarifa hiyo kuonekana kusainiwa na yeye wakati
hakuwahi kufanya hivyo.

“Mkurugenzi …hata hii saini
inaonekana ni ya yangu, lakini niseme kweli mimi sijawahi kuja kusaini
hili kablasha kama taratibu zinavyota na nashangazwa na hiki
kilichotokea humu, labda wenzangu katika kamati wao walisaini” alisema
Mwenyekiti huyo.

Hata hivyo, Mwenyekiti huyo wa
Halmashauri alitumia nafasi hiyo kuwahoji Wenyeviti wa kamati za kudumu
kama walihusika kusaini makablasha kama taratibu zinavyoagiza, ambapo
kwa pamoja walikataa kuwa hawakuwahi kupitia na saini taarifa
zilizowasilishwa.

Kutokana na mkanganyiko huo,
Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri hiyo, Athumani Masasi, alilazimika
kumnyanyua Mwandishi wa vikao ili kutoa ufafanuzi juu ya tuhuma za
kughushi saini.

Akijibu tuhuma hizo mwandishi huyo
wa vikao , licha ya kukiri kuwa utaaratibu huo umekuwa ukitumika mara
nyingi kutokana na makubaliano kati yake na Wenyeviti hao.

Akifafanua zaidi mara baada ya
kikao kumalizika, Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri hiyo, Masasi
alionekana kushangazwa na uamuzi wa madiwani kwani hata kama walibaini
kuwepo kwa kasoro walipaswa kuwasiliana na ofisi yake mapema na
kurekebisha.

“Kama mlivyomsikia CC …pale hakuna
fojali bali kilichotokea ni Madiwani kutafuta sababu tuu, baada ya
kutaka hoja ambazo hazikufuata taratibu ziingizwe kwenye ajenda za
kikao” .

Mapema kulionekana dalili za
kuvunjika kwa Baraza hilo kufuatia malumbano ya kikanuni kufuatia baadhi
ya Madiwani kutaka baadhi ya hoja zilizoibuliwa kwenye kikao cha chama
kuingizwa kama ajenda katika kikao hicho.

Baadhi ya taarifa hizo ambazo
Madiwani walitaka ziingizwe kama ajenda kwenye kikao hicho ni azimio lao
la kutaka taarifa ya fedha kiasi cha zaidi ya shiingi milioni 700 za
maendeleo ya upimaji ardhi kupitia ufadhili wa LIC.

Nyingine ni taarifa ya baadhi ya
watumishi wa Halmashauri kujigawia kwa upendeleo viwanja 19 bila kufuata
taratibu , pamoja na gari la Halmashauri lililotolewa msaada na
serikali ya Korea ya Kusini, kukamatwa na Taasisi ya Kuzuia na kupambana
na Rushwa (TAKUKURU) ikidaiwa kukodishwa kifisadi, huku dereva
aliyekuta akiendesha gari hilo si mtumishi wa umma.

Taarifa nyingine ilimuhusisha
mtumishi wa idara ya ardhi ndugu Joseph Towo kutumia watumishi na
mitambo ya kampuni yake kuendelea kupima maeneo kinyemela bila ya
kufuata taratibu na mitambo yake kukamatwa na diwani tarehe 13.10.19 na
kukiri kosa mbele ya kikao cha kamati ya fendha,uongozi na mipango.