Bashe abaini ufisadi wa bilioni 10 bodi ya korosho

Naibu
Waziri wa Kilimo, Hussein Bashe  ameiagiza Bodi ya Korosho nchini
kuhakikisha shilingi bilioni 10 kutoka hazina zilizotolewa kwa ajili ya
kununua mbolea na viwatilifu kwenye zao la korosho zinarudi hazina,
baada ya bodi hiyo kuzitumia kinyume na maelekezo ya serikali.

Naibu
Waziri Bashe aliyasema hayo katika ziara yake ya kukagua kontena zaidi
ya 350 za mbolea na viatilifu yaliyopo katika bandari kavu tatu ikiwamo
ya Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA) na Azam za jijini Dar es Salaam.

“Kuna
kampuni inaitwa Bajuta imepewa bilioni 4.5 kati ya bilioni 10 na Bodi
ya Korosho zilizotolewa na hazina kwenda kwa Kampuni ya Mbolea Tanzania
(TFC), wakati Bodi ya korosho inafanya maamuzi hayo hayakuwa ni maamuzi
ya serikali”- Alisema Bashe na kuongeza;


“Naagiza 
ufanyike ukaguzi maalum na ukaguzi wa uwezo kwa kampuni ya pembejeo na
viwatilifu ya Bajuta, juu ya mnyororo wa usambazaji pamoja na usambazaji
wa pembejeo katika sekta ya kilimo na ukaguzi huo usifanywe na Wizara
ya kilimo Bali ufanywe na hazina ili viongozi wote waliobadilisha
matumizi ya Sh. bilioni 10 zilizoelekezwa kwenda Kampuni ya Mbolea
Tanzania (TFC) wachukuliwe hatua  mara moja.”

Akifafanua
alisema TFC ilipewa jukumu la kuagiza mbolea na dawa aina ya Salfa ili
iweze kuuzwa kwa wakulima kwa bei nafuu, lakini ilipokea Sh. bilioni
moja kati ya 10 iliyotolewa na Hazina na hivyo bodi hiyo kuwakwamisha
kutimiza malengo ya serikali.

Alisema mwaka mmoja sasa TFC, bandari kavu hizo zinashikilia kontena zaidi ya 350 zenye mbolea na Salfa.
 
“Rais
Dk. John Magufuli alipotoa fedha hizo kwenda TFC alikusudia wakulima
wapate unafuu wa mbolea na viatilifu ili kuwaboreshea kilimo chao,
nasisitiza kwamba Kampuni ya Bajuta irudishe Sh. bilioni 4.5 mali ya
serikali,” alisema Bashe.