Magari mawili yagongana jijini mbeya

Mnamo
tarehe 17.02.2020 majira ya saa 03:00 usiku wa kuamkia leo huko eneo la
Ilomba, Kata ya Ilomba, Tarafa ya Iyunga, Jijini Mbeya katika barabara
kuu ya Mbeya – Tunduma, Gari lori tanker la mafuta lenye namba za
usajili T.720 DHV na Tela T.520 CCY likiendeshwa na ABUBAKAR MOHAMED
[32] Mkazi wa Dar es Salaam likitokea Dar es Salaam kuelekea nchini
Zambia likiwa limebeba mafuta Petrol na Diesel liligongana uso kwa uso
na Gari ndogo yenye namba za usajili T.536 DDM aina ya Toyota Carina
iliyokuwa inatokea Mbeya Mjini.




Katika ajali hiyo dereva wa gari ndogo T.536 DDM Toyota Carina amejeruhiwa na anaendelea na matibabu. 

Chanzo cha ajali hiyo ni mwendo kasi wa magari yote mawili katika eneo la makazi ya watu.

 Aidha
katika ajali hiyo magari yote mawili yameharibika na Tanker la Mafuta
liliacha njia na kwenda kugonga maduka ya bidhaa mbalimbali yaliyopo
kando kando ya barabara.

Jeshi
la Polisi kwa kushirikiana na vyombo vingine vya ulinzi na usalama lipo
eneo la tukio kuhakikisha mafuta yaliyopo katika gari lililopata ajali
yanahamishiwa kwenye gari lingine bila kusababisha madhara yoyote ikiwa
ni pamoja na jitihada za kuliinua tanker la mafuta lililoacha njia na
kupinduka.