Viwanda nchini vyatakiwa kutumia njia bora za uchinjaji na uchunaji ngozi

 

Kaimu Msajili Bodi ya Nyama Tanzania  Imani Sichalwe (alievaa koti la suti) akiwa na Mkuu wa Idara wa Mifugo halmashauri ya Manispaa ya Shinyanga Kwenye Ukaguzi wa Maendeleo ya ujenzi wa kiwanda cha Nyama cha halmashauri ya Manispaa Shinyanga,akiwa ameambatana na Mkuu wa Idara ya Mifugo Abdallah Chamzimu  
 Muonekano wa Kiwanda cha Kisasa cha Nyama cha halmashauri ya manispaa ya Shinyanga.
Na.Vero Ignatus

Viwanda vya Nyama Nchini vyatakiwa kutumia njia bora za kisasa za Uchinjaji na uchunaji ngozi,jambo litakalosaidia Kuongeza uzalishaji wa nyama na bidhaa zake katika viwango vya Ubora ili kukidhi soko la ndani na nje ya nchi.

Hayo yamesemwa na Imani Sichalwe Kaimu Msajili wa Bodi ya Nyama Tanzania,  alipotembelea na Kukagua Maendeleo ya ujenzi wa kiwanda cha Kisasa cha Nyama cha halmashauri ya manispaa ya Shinyanga.

 Sichalwe amesema uwepo wa ongezeko la kasi la uanzishwaji wa viwanda hivyo vya vyama ,umekuwa ni ukombozi mkubwa kwa wafugaji ambao wamekuwa wakisumbuka kwa muda mrefu kutafuta masoko ya mifugo yao.

Amesema nyama itakayozalishwa kwenye kiwanda hicho cha halmashauri ya manispaa ya Shinyanga, itakuwa katika viwango vya ubora kutokana na uwepo wa miundombinu ya kisasa, ikiwemo kuwatumia wataalamu wabobezi wa masuala ya mifugo ambao watasimamia uendeshaji wa shughuli za uzalishaji kwenye kiwanda hicho.

Aidha ameshauri uongozi wa kiwanda hicho kuwasiliana na uongozi wa kiwanda cha ngozi cha Karanga Moshi, ili kupata Fursa ya kuuza ngozi kwenye kiwanda hicho ambacho kitachukua asilimia sabini na tano ya ngozi zote, zinazozalishwa nchini kwa ajili ya utengenezaji wa bidhaa.

Kiwanda hicho cha nyama cha halmashauri ya manispaa ya Shinyanga, kinatarajiwa kuanza uzalishaji November 30 Mwaka huu ambapo kinatarajiwa kuchinja ng’ombe 500 kwa siku na mbuzi, 1000 na kitahudumia Masoko ya ndani na nje ya nchi.