Wanaoishi kwenye mazingira magumu hatarini kukumbwa na corona

 


Na
Mwandishi Wetu, 
Arusha.

Wakati serikali ikitoa elimu juu ya kujikinga na
ugonjwa wa homa kali ya mapafu (CORONA), kundi la watoto wa mitaani
limesahaulika hali inayohatarisha afya na maisha yao.

Watoto hao hawana makazi maalumu kama ambayo
mwandishi wa habari hii amewakuta wakizurura maeneo mbalimbali ya mjini wa
Arusha na baadaye majira ya usiku kulala nje ya maduka ya wafanyabiasha katika
ya mji huo hivyo ni muhimu sana kupatiwa elimu ya afya ya jinsi ya kujingika na
ugonjwa huo.

Wakizungumza na APC Blog kwa masharti ya kutotajwa
majina yao hali wala kupigwa picha baadhi ya watoto hao walisema hawajwahi
kupatiwa elimu yoyote juu ya ugonjwa huo na kwamba wana uhitaji wa kujua jinsi
ya kujikinga ili wasikumbane nao.

“Sisi tunaona watu wakipita katika maduka na huko
standi kuwaelimisha juu ya Corona, lakini sisi hatujawahi kuitwa au kukusanywa
mahali tukapewa elimu, naona ni kwa sababu hatuna makazi maalumu ya kuishi”
Alisema Elias John ambaye siyo jina lake kamili.

“Kama unavyotuona hapa hatuna maski, ndoo za maji
kwa ajili ya kunawa mikono, hatuna sabuni wala zile dawa za kujipaka mikononi
(akimaanisha vitakasa mikono), kwa hiyo tunaiomba serikali itusaidie na sisi
kwa sababu pia tunaishi mazingira hatarishi” Alisema Peter Godgfrey (siyo jina
lake kamili)

Baadhi ya wafanyabiashara katika maeneo ya standi
kuu walisema kuna umuhimu kwa kundi hilo kupatiwa elimu juu ya Corona kwani
wamekuwa wakiishi maisha ya kawaida kama walivyokuwa wakiishi awali licha ya
kuwepo kwa janga hili.

“Hata wewe hapa ulipo unaweza kuona wanavyopitapita,
umeona hata mmoja amevaa barakoa?, hawajui lolote kuhusu kuchukua tahadhari, ni
vyema idara inayowasimamia (Ustawi wa jamii) iwape elimu” Alisema mmoja wa
wafanyabiashara ambaye hakutaka jina lake liandikwe.

Afisa Ustawi wa jamii jiji la Arusha alipotakiwa
kuzungumza kuhusu suala hilo, alisema yeye siyo msemaji wa suala hilo licha ya
mwandishi kumwambia Mkurugenzi wa jiji amemruhusu kulisemea lakini alisema
anataka kibali cha maandishi kutoka kwa mkubwa wake wa kazi.

“Unajua dada haya mambo ya kupewa maelekezo kwa
mdomo siyo sahihi, ningeomba nipate kimaandishi ili baadaye niwe salama, kwa
kuwa kiutaratibu Mkurugenzi ndiye msemaji wa kila jambo linalohusu idara zote
zilizopo ofisi ya halmashauri ya jiji” Alisema