Waziri mkuu: tozeni bili za maji zisizowaumiza wananchi

 

WAZIRI
MKUU, Kassim Majaliwa ameiagiza Wizara ya Maji ifuatilie utendaji wa
Mamlaka zilizopewa dhamana ya kusimamia miradi ya maji katika maeneo
mbalimbali nchini na ihakikishe kwamba bili wanazotozwa wananchi
zinakuwa na uhalisia na si kuwaumiza.


Ametoa
agizo hilo baada ya kuibuka wimbi la malalamiko kutoka kwa wananchi
kuhusu upandaji wa bili za maji ambao hauna uhalisia kwa sababu Serikali
ndiyo inayotoa fedha za miradi hiyo nchini.”Serikali haitakubali wala
haitoruhusu mwananchi anatozwa gharama kubwa za maji.”

Waziri
Mkuu ameyasema hayo leo (Alhamisi, Septemba 12, 2019) Bungeni jijini
Dodoma katika kipindi cha maswali ya papo kwa papo kwa Waziri Mkuu
wakati akijibu swali la Mbungewa Viti Maalumu, Mariam Kisangi, aliyetaka
kujua kauli ya Serikali kuhusu suala hilo.

“Yako
maeneo ambayo mamlaka zilizopewa dhamana ya kusimamia miradi ya maji
kumejitokeza wimbi la mabadiliko ya kuhusu kupanda kwa bei za bili,
mfano wilayani Maswa mkoani Simuyu bei imeongezeka kutoka sh. 5,000 hadi
28,000 kwa mwezi.”

“Bei
hizo hazina uhalisia na hakuna sababu ya mamlaka kuzoza bei kubwa kiasi
hicho na kuwafanya wananchi washindwe kumudu kulipia bili zao, wakati
Serikali ndio imetoa fedha za kugharamamia uanzwishwaji wa miradi hiyo
na haijadai kurudishiwa fedha hizo.”

Waziri
Mkuu amesema Wizara ya Maji kupitia Mamlaka ya Udhibiti wa Nishati na
Maji (EWURA) ifuatilie bei za bili wanazotozwa wananchi ili
kujiridhishwa kwamba zinazingatia uwezo wa wananchi wengi kuzilipa hasa
wale wa vijijini.

Wakati
huo huo, Waziri Mkuu amewaagiza Wakuu wa Mikoa, Wilaya, Wakurugenzi wa
Halmashauri, Maafisa Kilimo na Maafisa Biashara kote nchini wasimamie
katika masoko yote na wajirishe iwapo vipimo vinavyotumika ni sahihi
kwani lumbesa haikubaliki.

Ametoa
agizo hilo wakati akijibu swali la Mbungewa Jimbo la Mlalo, Rashid
Shangazi aliyetaka kupata kauli ya Serikali kuhusu hatua zilizochukuliwa
katika kudhibiti unyonyaji wanaofanyiwa wakulima kupitia ufungaji wa
mazao unaozidi viwango.

Waziri
Mkuu amesema wanunuzi wa mazao mbalimbali lazima wafuate sharia, kanuni
na taratibu za manunuzi ya mazao husika. “Maafisa Kilimo wasimamie
biashara hiyo na waendeshe operesheni kwenye maeneo ya masoko ili
kujirishana vipimo vinavyotumika.”

Amesema
ni muhimu zaidi kutumia mizani ambayo haina utata ili kuwawezesha
wakulima kuweza kunufaika kutokana na kilimo na kwamba suala la
waununuzi kutumia vipimo visivyosahihi kama lumbesa halikubaliki.

Akijibuswali
la Mbunge wa Sumve, Richard Ndasa aliyetaka kupata kauli ya Serikali
kuhusu kuhusu suala la ununuzi wa zao la pamba, Waziri Mkuu amesema
Serikali imelifanyia kazi suala hilo na tayari zaidi ya tani 200,000
zimeshanunuliwa ambayo ni sawa na asilimia 80.

Waziri Mkuu amewahakikishia wakulima wa zao la pamba kwamba pamba yote iliyosailia majumbani itanunuliwa.

(mwisho)
IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU,