Mbunge akiri watu kupotea loliondo na wengine kukimbilia kenya

Mbunge wa Ngorongoro Emmanuel Ole Shangai

 

Na Mwandishi Wetu, Loliondo.

Kufuatia zoezi linaloendelea la uwekaji wa alama za mipaka katika pori tengefu la Loliondo Mbunge wa Jimbo la Ngorongoro Emmanuel Ole Shangai amethibitisha baadhi ya wakazi wa Tarafa ya Loliondo na Sale  kukimbilia nchi jirani ya Kenya huku wengine wakipotea na hawajulikani walipo hadi hivi sasa.

Akizungumza na waandishi wa habari hizi, mbunge wa jimbo hilo amesema jumla ya watu 31 wamejeruhiwa na wapo nchini Kenya kwa ajili ya matibabu baada ya kukosa Fomu Namba Tatu (PF3) kwa ajili ya matibabu kwa kuhofia usalama wao kwa kile kinachoendelea katika eneo hilo.

Akizungumzia hali za majeruhi hao amesema baadhi yao wamevunjika miguu na mikono huku wengine wakipata majeraha sehemu mbalimbali za miili yao ikiwemo mabegani na kwamba watarejea nchini baada ya afya zao kuimarika.

 

“Mkuu wa Mkoa katoa taarifa yake, lakini na mimi nasema hii taarifa yangu ni ya kweli, na hata majina ya majeruhi ninayo, kwa ujumla nina kila details (maelezo) ya kina juu yao, kwa hiyo sina shaka na taarifa hii ninayoitoa” Alisema Ole Shangai.

Aidha amesema kuwa miongoni mwa watu waliokamatwa na hadi sasa hawajulikani walipo toka Juni,9 mwaka huu 2022 ni pamoja na baadhi ya madiwani na viongozi wengine akiwemo Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Ngorongoro, ambao waliitwa kuhojiwa na hivyo kuitaka serikali kuwaachia huru mara moja kwani kitendo hicho kinazidi kuleta wasiwasi na hofu kwa wananchi wa eneno hilo.

Ole Shangai amesema hali hiyo imepelekea kushindwa kuhudhuria vikao vinavyoendelea kwa sasa bungeni na kwamba anatarajia kupelekea suala hilo kama hoja binafsi bungeni kwa lengo la kutafuta amani miongoni mwa wananchi na serikali yao.

Mkuu wa Mkoa wa Arusha John Mongella ambaye pia Mwenyekiti wa Kamati ya Ulinzi na Usalama wa Mkoa huo amesema zoezi la uwekaji alama katika eneo hilo linaendelea kufanyika kwa utulivu na hakuna vurugu zozote licha ya kukiri kutokea kifo cha askari polisi mmoja aliyeuawa na wananchi katika zoezi hilo.

Amesema mpango wa serikali ni kupunguza eneo la kilometa za mraba 1500 ili liwe hifadhi pekee na kwamba hakuna mwananchi hata mmoja ambaye ataondolewa katika eneo hilo.