Uamuzi kesi ya tundu lissu kutolewa leo


Leo
Septemba 9, 2019 Mahakama Kuu ya Tanzania Dar es salaam, inatarajia
kutoa uamuzi wa kesi ya aliyekuwa Mbunge wa Singida Tundu Lissu, dhidi
ya Spika wa Bunge la Tanzania Job Ndugai.




Pamoja
na mambo mengine, Lissu ameiomba mahakama kutoa zuio la muda kwa
mlalamikiwa wa kwanza Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano, Job Ndugai,
kusitisha tukio la kumwapisha Mtaturu katika Mkutano wa Bunge ulioanza
Jumanne iliyopita  jijini Dodoma.

Hata hivyo, kutokana na Mahakama kuahirishwa jioni ya Agosti 29, mwaka
huu bila kutoa uamuzi, Bunge lilimwapishwa mbunge mpya wa jimbo hilo,
Miraji Mtaturu, aliapishwa siku hiyo kwa mujibu wa ratiba iliyopangwa na
Bunge ya mkutano huo.

Katika maombi hayo namba 18 ya mwaka 2019, dhidi ya Spika Job Ndugai na
Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG), Lissu anaomba kibali cha kufungua
shauri la maombi maalum ikiwamo kumtaka Spika awasilishe mahakamani
taarifa aliyoitoa bungeni ya kumvua ubunge ili iweze kupitiwa na
Mahakama na kufanyiwa maamuzi.

Kwa mujibu wa hati ya maombi hayo mlalamikaji anaomba mahakama kuitishwa
uamuzi uliofanywa na Spika, kuufanyia uchunguzi na kukiwasilisha.

Wakili Peter Kibatala alidai kuwa sababu kubwa ya kuomba kibali ni
kutokana na kazi ya mahakama kupitia nyaraka kama zinafaa kusikilizwa
kama mlalamikaji anavyoomba.

“Katika kipindi cha miaka saba iliyopita Lissu alikuwa anafanyakazi zake
za uwakili wa wananchi vyema, lakini alishambuliwa kwa risasi na
kutibiwa jijini Nairobi, nchini Kenya na baadaye akahamishiwa Ubelgiji.”

Akifafanua zaidi wakili alidai kuwa Lissu hakuwahi kupewa taarifa za kutenguliwa ubunge wake amesikia barabarani.