Wazazi wahitimu darasa la saba washauriwa kupeleka watoto wao mafunzo ya awali kidato cha kwanza, ili kuepuka makundi hatari ya mtaani

 Na Seif Mangwangi, Arusha

Wazazi na walezi wa wanafunzi wanaohitimu darasa la saba wameshauriwa kupeleka watoto wao kwenye mafunzo ya awali ya kidato cha kwanza (Pre-form one), ili kuwaepusha na makundi ya mtaani ambayo ni hatari.

Wahitimu wa darasa la saba wakiwa kwenye mavazi rasmi yaliyobuniwa shuleni hapo

Akizungumza kwenye mahafali ya kwanza ya shule ya msingi Shining star, Afisa Elimu Msingi Wilaya ya Arumeru, Hussein Mgawe amesema elimu ambayo watoto wameipata ni vizuri wakaiendeleza kabla hawajasahau.

“Nawashauri wazazi pelekeni watoto shule ili waweze kuwa tegemeo lenu hapo baadae. elimu sio mpaka kupata ajira, itakiwezesha kupata ujuzi wa ziada, pia wapelekeni pre form one ili kuwajengea uwezo wanapoanza rasmi kidato cha kwanza mwakani,”amesema.

Pia amesema kuna faida nyingi za watoto kusoma ikiwemo kupata ajira na kwamba ajira sio  mpaka uende serikalini hata huko mtaani kuna pesa nyingi na kuwazidi hata wanaoajiriwa serikalini.

“Unachotakiwa kujua ni kwamba mtu yoyote ambaye hajapata elimu hawezi kuwa na ujuzi huko mtaani kama aliyepata elimu, kwa hiyo tupeleke watoto shuleni,”amesema.

Amesema katika mitihani ya Mock ya darasa la saba na la nne,  shule ya msingi, shining star iliweza kufanya vizuri sana na kuzidi shule zingine nyingi hivyo anatumaini katika mtihani wa mwisho wa darasa la saba itashika nafasi ya juu zaidi kitaifa.

Afsa Elimu Hussein Mgawe mwenye tai nyekundu akiwa katika picha ya pamoja na wanafunzi wa jamii ya kifugaji wanasoma shuleni hapo

“Napenda kutoa wito kwa wanafunzi wanaobaki kuendelea kujisomea mambo yote yanayofundishwa lakini na wazazi  mjitahidi kusaidia hawa watoto wetu katika malezi ili kuweza kufaulu na kushika nafasi za juu kitaifa,” amesema.<

Mzazi wa Neema Sironga, Jonais Mambali akimpongeza mwanae kwa kuibuka mshindi wa pili wa jumla kwa masomo yote darasa la saba shuleni hapo. Neema pia ndio mshindi wa kwanza katika somo la Sayansi na teknolojia

Amewataka wanafunzi wanaohitimu kusoma vizuri na kuhakikisha wanaelewa vyema masomo yao na baadae wawe madaktari wazuri watakaoweza kuhudumia jamii katika kutibia maradhi mbalimbali.

Kwa mujibu wa Mkurugenzi Mkuu wa Shule ya Msingi Shining Star, Lomnyak Pipiyo  shule hiyo ilianzishwa mwaka 2015 ina wanafunzi zaidi 300 kuanzia na chekechea hadi darasa la saba.