Naibu waziri mhe. katambi awasihi wananchi shinyanga kupuuza watu wanaotumia rushwa nyakati za uchaguzi.

Na Mapuli Misalaba, Shinyanga

Naibu waziri ofisi ya waziri mkuu kazi,
vijana, ajira na watu wenye ulemavu ambaye pia ni Mbunge wa jimbo la Shinyanga
mjini Mhe. Paschal Patrobas Katambi amewaomba wanananchi  kutowapa nafasi watu watakaoomba nafasi ya
uongozi kwa njia ya rushwa.

Ameyasema hayo leo wakati akizungumza
kwenye mkutano wa wajasiliamali ambao umehudhuriwa na viongozi wa serikali,
viongozi wa CCM pamoja na wadau mbalimbali, ambao umefanyika katika ukumbi wa
ofisi za CCM Mkoa wa Shinyanga.

Mhe. Katambi amewasihi wananchi hasa
wakazi wa jimbo la Shinyanga mjini kutowapa kura watu ambao hujitokeza nyakati
za uchaguzi kugombea nafasi ya uongozi kwa ajili ya maslahi yao binafsi.

“Tunao wajibu mkubwa sana wa kuwa na uchungu na
Shinyanga yetu na kuangalia maendeleo yetu tusiwape nafasi viongozi watakaotaka
madaraka kwa ajili ya maslahi yao binafsi matokeo yake wataiacha Shinyanga
ikiwa hoi bila maendeleo, hii Shinyanga bila kuwa na uchungu na dhamira ya dhati
ya kujitoe hatuwezi kuihudumia mimi nimeingia kwenye jimbo hili tukiwa hatuna
hata uwanja wa ndege zilikuwa ni ahadi tu lakini sasa hivi uwanja ule tumepata
fedha shilingi Bilioni 49 kazi inafanyika na vijana wetu lazima wapate ajila”.

“Kura yako ndiyo maendeleo yako unaweza kufurahi leo
kwa kupata elifu kumi elfu ishilini lakini madhara utakayoyapata baada ya hapo
ukienda Hospitali dawa hakuna vituo vya afya viko mbali, barabara mbovu hiyo
laki moja yako haitakupeleka popote na watakaoumia ni watoto wetu na sisi
wenyewe kwahiyo kama tutachagua viongozi kwa rushwa na fedha tutajifurahisha
sisi kundi dogo lakini waliowengi wataumia nawaambia hili kwa maslahi pengine
kama hutoumia wewe wahurumie watoto wako”amesema Mhe. Katambi

Aidha Mbunge Mhe. Katambi amesema
ataendelea kushughulikia changamoto zinazowakabili wakazi wa jimbo la Shinyanga
mjini huku akiwaomba kuendelea kutoa ushirikiano kwa viongozi mbalimbali
wakiwemo madiwani ili kuchochea maendeleo katika jimbo hilo.

Naibu waziri huyo  amewahakikishia wananchi kuwa suala la mikopo serikali
imelifanyia kazi ambapo itaanza kutolewa Mwaka kesho 2024 baada ya  maboresho kufanyika  na kwamba Halmashauri zote zitatoa mikopo hiyo
kwa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu zilizowekwa.

Akizungumza mkuu wa Wilaya ya Shinyanga
Mhe. Johari Samizi naye amewahakikishia wananchi kuendelea kusimamia miradi
yote ya maendeleo ambayo imelenga kutatua kero za wananchi pamoja na kuchochea
uchumi katika jamii na Taifa kwa ujumla.

Kwa upande wake naibu meya wa Halmashauri
ya Manispaa ya Shinyanga Mhe. Zamda Shaban akizungumza kwa niaba ya madiwani wa
Manispaa hiyo amewaomba wananchi kuendelea kutoa ushirikiano katika utatuzi wa
changamoto ikiwa ni sehemu ya kuunga mkono maono ya serikali ya awamu ya sita
inayoongozwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Baadhi ya wajasiliamali waliohudhuria
mkutano huo wamemshukuru kwa elimu iliyotolewa huku wakimpongeza  Naibu waziri ofisi ya waziri mkuu kazi,
vijana, ajira na watu wenye ulemavu ambaye pia ni Mbunge wa jimbo la Shinyanga
mjini Mhe. Paschal Patrobas Katambi kwa kuendelea kuwajali katika mambo
mbalimbali ya maendeleo.

 

Naibu waziri ofisi ya waziri mkuu kazi,
vijana, ajira na watu wenye ulemavu ambaye pia ni Mbunge wa jimbo la Shinyanga
mjini Mhe. Paschal Patrobas Katambi akizungumza kwenye mkutano huo leo Alhamis
Disemba 21,2023 katika ukumbi wa CCM Mkoa wa Shinyanga.

Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga Mhe. Johari
Samizi akizungumza kwenye mkutano huo leo Alhamis Disemba 21,2023. 
 

Mkurugenzi mtendaji wa shirika la Child
Support Tanzania akitoa elimu kwa wajasiliamali katika mkutano huo leo Alhamis
Disemba 21,2023. katika ukumbi wa CCM Mkoa wa Shinyanga.

Katibu wa CCM Mkoa wa Shinyanga Bi. Odilia
Batimayo akizungumza kwenye mkutano huo wa wajasiliamali  Alhamis Disemba 21,2023. katika ukumbi wa CCM
Mkoa wa Shinyanga.