Tira yasisitiza wakulima na wafugaji kukata bima ya kilimo

MAMLAKA YA USIMAMIZI WA BIMA NCHINI (TIRA) YASISITIZA WAKULIMA NA WAFUGAJI KUKATA BIMA YA KILIMO

Meneja wa TIRA Kanda ya Kaskazini Eliezer Rweikiza akitoa ufafanuzi kuhusiana na Bima ya Kilimo katika maonyesho ya 26 Kanda ya kaskazini Njiro Mkoani Arusha.

Paulo Makanja ni Mwanasheria Mwandamizi kutoka TIRA:amesisitiza wakulima wanaodai malipo ya Bima wafike banda la TIRA kwaajili ya msaada zaidi

Meneja wa TIRA kanda ya Kaskazini Eliezer Rweikiza akisisitiza kwajambo mteja kama anavyoonekana katika picha,kushoto kwake ni Paulo Makanja ni Mwanasheria Mwandamizi kutoka TIRA

NaVero Ignatus, APC BLOG, ARUSHA

Mamlaka ya usimamizi wa Bima nchini TIRA imewataka wananchi wanaojihusisha na kilimo pamoja na ufugaji kukatia bima huduma zao na kujikinga na majanga mbalimbali ambayo yanaweza kuwakuta na kwamba huduma hiyo inapatikana hivi sasa katika viwanja vya nane nane kote nchini.

Akizungumza katika viwanja vya nane nane njiro jijini hapa, Meneja wa TIRA Kanda ya Kaskazini Eliezer Rweikiza amesema yapo makampuni ambayo ni mahususi kwa kutoa huduma katika sekta ya Kilimo na Mifugo na sio kampuni zote.

Amesema hivi karibuni Mamlaka hiyo iliendesha mafunzo kwenye vikundi takribani 50 vinavyojumuisha VICOBA,SACOS,AMCOS, pamoja na wajasiriamali ambao walielezwa namna ya upata hizo huduma ya bima ya kilimo na mifugo.

Rweikiza amesema vijiji ambavyo ofisi yake ya kanda ya kaskazini imeweza kutoa elimu ya bima ni vya kutoka katika Mikoa ya Tanga ambapo vijiji 34 katika wilaya za Muheza, Korogwe na Tanga mjini vilipatiwa elimu, na vijiji14 katika wilaya za Babati na Hanang’ mkoani Manyara

Rweikiza amesema kuwa mkulima anapokata bima ya kilimo inamkinga na majanga ambapo ikitokea akapata hasara anafidiwa na kampuni husika vilevile mkulima anakuwa amekinga uchumi wake usitetereke kutokana na hasara aloipata.

” Kwa hiyo hii bima ni muhimu sana kwa wote wanaolima kilimo kikubwa au kilimo kidogo ,yote haijalishi huduma ya bima ipo inahusika ,kwahiyo tunawataka sana wananchi hasa kanda ya kaskazini wakate bima ya Kilimo na Mifugo,”anasisitiza

Mwanasheria Mwandamizi kutoka TIRA Paul Makanja amesema kuwa katika msimu huu wa nanenane watashughulika na malalamiko ya wananchi ambao wanayadai makampuni mbalimbali ya bima ambapo madai yao hayaja shughulikiwa hadi sasa,na kuwasaidia namna gani wanaweza kulipwa madai yao hasa yale yanayolipika.

Sambamba na hayo amesema kuwa watashughulikia namna ya kutoa ushauri kwa kwa watu ambao wanahitaji kusajili makampuni yao katika kufanya shughuli za Bima,kwa maana ya wale wanaohitaji kufanya udalalali,Mawakala,sambamba na wale wanaotaka kufanya kazi ya ukadiriaji hasara za Kibima

Amesema kuwa miongoni mwa kazi kubwa ya mamlaka hiyo ni kuhakikisha kuwa soko la Bima linakuwa linaendeshwa kwa uhuru,wazi na kuwa faida kwa watu ambao ni wanufaika katika shughuli za Bima.

Ametoa wito kwa wakazi wa kanda ya kaskazini kujitokeza kwa wingi katika maonyesho hayo kwani wamegundua ya kwamba uwelewa wa bima bado haujawa mkubwa hivyo wananchi watembelee banda la TIRA sambamba na mabanda mengine yanayojihusisha na shughuli za bima katika mtaa wa Bima.